TANZANIA KUTOKUWA MWENYEJI AFCON 2017

 sehemu ya uwanja wa uhuru ambao upo kwenye matengenezo

Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limefahamishwa na Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) kuwa Tanzania haitaweza kuwa mwenyeji wa Fainali za Afrika- AFCON 2017 kwa kuwa haijawahi kuandaa fainali zozote za vijana Afrika. Fainali hizo ni zile za vijana wenye umri chini ya miaka 17 na 20.

Hivyo, TFF inaelekeza nguvu zote katika kuandaa Fainali za Afrika kwa vijana wenye umri chini ya miaka U17 mwaka 2019.

Tunapenda kuchukua fursa hii kumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanazania, Jakaya Kikwete kwa kututia moyo katika kuomba uenyeji wa AFCON 2017.

Pia tunamshukuru Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk Fenella Mukangara kwa juhudi binafsi alizozionyesha katika jitihada za Tanzania kuomba uenyeji  wa AFCON 2017.

TFF inaamini kwa dhati kuwa uenyeji wa Afrika U17 2019 utaifungulia Tanzania milango ya kuandaa mashindano makubwa zaidi.

WANYARWANDA KUCHEZESHA MECHI YA STARS
Waamuzi kutoka Rwanda ndiyo watakaochezesha mechi ya Kalenda ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) kati ya Taifa Stars na Benin itakayofanyika Jumapili (Oktoba 12 mwaka huu) jijini Dar es Salaam.

Hakizimana Louis ndiye atakayeongoza waamuzi hao wa FIFA kwa kupuliza filimbi kwenye mechi hiyo itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 11 jioni. Atasaidiwa na Simba Honore na Niyitegeka Jean Bosco.

Mechi hiyo itatanguliwa na ile ya viongozi wa dini- Kiislamu vs Kikristo kudumumisha upendo, amani na ushirikiano itakayoanza saa 9 kamili alasiri. Tiketi za elektroniki zitakazotumika kwa mechi hiyo tayari zimeanza kuuzwa kwa kiingilio cha sh. 4,000 na sh. 10,000.

Wakati huo huo, Kocha Mart Nooij ameongeza wachezaji watatu kwenye kikosi cha Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager ili kukiongezea nguvu kwa ajili ya mechi hiyo.

Wachezaji walioongezwa ni Jonas Mkude na Joram Mgeveke kutoka timu ya Simba, na Gadiel Michael wa Azam.

Post a Comment

Previous Post Next Post