TANZANIA KUWA KITOVU CHA UMEME KASKAZINI, KUSINI MWA AFRIKA Ø Ni baada ya kukamilika Mradi Mkubwa wa Backbone Kilovoti 400 Ø Ujenzi wake kugharimu Bil. 760 Ø Rais Kikwete kuuzindua Novemba




Na Veronica Simba – Aliyekuwa Dodoma
Tanzania inatarajiwa kuwa kitovu cha uunganishaji wa umeme uliopo Kaskazini na Kusini mwa Afrika mapema mwakani baada ya kukamilika kwa mradi wa ujenzi wa njia kuu ya umeme wa Kilovoti 400 yenye urefu wa Kilomita 670 kutoka Iringa hadi Shinyanga.
Mradi huo unaojulikana kama Backbone na uliopangwa kukamilika mwezi Aprili mwakani, unatarajiwa kuzinduliwa na Rais Jakaya Kikwete Novemba mwaka huu na utagharimu takribani Dola za Marekani Milioni 455 sawa na shilingi bilioni 760 za kitanzania.
Hayo yalibainika mwishoni mwa wiki iliyopita wakati wa ziara ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo aliyoifanya kwa lengo la kukagua maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo katika vijiji vya Mlowa, Nala na Mbwanga mkoani Dodoma.
Akihitimisha ziara hiyo, Waziri Muhongo aliwaambia waandishi wa habari kuwa mradi wa Backbone utakapokamilika utaziunganisha gridi za nchi za Kenya kwa upande wa Kaskazini na Zambia upande wa Kusini Magharibi. Kwa kuunganisha gridi hizo, kutaifanya Tanzania kuwa “kitovu cha uunganishaji wa umeme uliopo Kaskazini  na Kusini mwa Afrika (East and Southern Africa Power Pool).
Alisema, mradi huo pia utahusika kusambaza umeme katika vijiji vilivyo kando kando ya njia kuu ya umeme ambayo itaunganisha upande wa Kusini mwa nchi ambako kunatarajiwa kuwa na vyanzo vingi vya umeme kama Kiwira, Mpanga, Ruhudji, Mchuchuma na Rumakali.
Aidha, alisema kuwa mradi wa Backbone utaunganisha upande wa Kaskazini wenye matumizi makubwa ya umeme yanayotokana na kuwepo kwa migodi ya madini na viwanda mbalimbali.
Vilevile, Profesa Muhongo alisema Backbone itaongeza upatikanaji wa umeme wa uhakika upande wa Kaskazini na Magharibi mwa Tanzania na kuwezesha watu wengi kufungiwa umeme hasa vijijini na hivyo kuharakisha mpango wa taifa wa kuinua uchumi na kupunguza umaskini.
Akizungumzia maendeleo ya utekelezaji wa mradi huo, Profesa Muhongo alisema ameridhishwa na utekelezaji wake na kuongeza kwamba ana imani mradi utakamilika kwa wakati na kwa ubora unaotakiwa.
“Serikali tunaposema tumedhamiria kuzalisha umeme mwingi na wa uhakika hatutanii. Mradi umeanza vizuri na nina imani utakamilika kama ulivyopangwa,” alisisitiza.
Naye Kamishna Msaidizi wa Nishati, Sehemu ya Umeme, Mhandisi Innocent Luoga alisema utekelezaji wa mradi wa Backbone umegawanyika katika sehemu nne. Sehemu hizo ni pamoja na ujenzi wa njia ya umeme wa Kilovolti 400 kutoka Iringa hadi Dodoma yenye urefu wa kilomita 225 ambayo inajengwa na Mkandarasi KEC International Limited na ujenzi wa njia ya umeme wa Kilovolti 400 kutoka Dodoma hadi Singida yenye urefu wa kilomita 217 inayojengwa na Mkandarasi Jyoti Structures Limited.
Alizitaja sehemu nyingine kuwa ni njia ya umeme wa Kilovolti 400 kutoka Singida hadi Shinyanga yenye urefu wa kilomita 228 inayojengwa na KEC International Limited pamoja na upanuzi wa vituo vya kupoozea umeme vya Iringa, Dodoma, Singida na Shinyanga, vinavyojengwa na GSE&C & HYOSUNG.
Mhandisi Luoga alisema ujenzi wa mradi huo umefadhiliwa kwa mkopo kutoka Washirika wa Maendeleo wa Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB), Shirika la ushirikiano la Japani (JICA), Benki ya Jumuiya ya Ulaya (EIB) na Benki ya Korea kupitia EDCF.
Kuhusu ulipaji fidia kwa wananchi waliopitiwa na mradi, Mhandisi Luoga alisema mchakato wa kutambua sehemu ambapo njia kuu ya umeme itapita na kuangalia watu watakaoathiriwa na mradi ulishafanyika.
Alisema serikali ililipa jumla ya shilingi bilioni 22.5 kama fidia kwa wananchi husika, zoezi ambalo lilifanyika kati ya mwaka 2009 na 2010. Aidha, alisema kuwa serikali inatekeleza ujenzi wa majengo mapya ya kisasa kwa taasisi na mashirika ya dini yaliyopitiwa na mradi kama ofisi za serikali za vijiji, shule, misikiti, makanisa, vituo vya polisi na majosho ya ng’ombe.
Aidha, Mhandisi Luoga alisema mradi pia utajenga njia za umeme wa msongo wa kilovolti 33 kwa ajili ya wananchi wanaoishi kando kando na njia kuu ya umeme kwa ufadhili wa NORAD, SIDA na Serikali ya Tanzania kupitia Wakala wa Umeme Vijijini (REA).
Aliongeza kuwa mradi huo utatekelezwa na REA pamoja na Shirika la Umeme nchini (TANESCO) ambapo jumla ya vijiji 91 vitafaidika na mpango huo.
Mradi wa Backbone ulianza kutekelezwa Novemba 2013 chini ya Mshauri Mwelekezi (OISF) – Fitchner kutoka Ujerumani kwa kushirikiana bega kwa bega na Wahandisi wa TANESCO.
-- 



Post a Comment

Previous Post Next Post