Mabadiliko ya teknolojia pamoja na kuboreshwa kwa
bandari zilizo chini ya Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari nchini (TPA) zimeanza
kuzaa matunda baada ya meli nyingine kubwa yenye urefu wa mita 209 kutia nanga
Bandari ya Mtwara.
Ujio wa meli hiyo iliyotia nanga katika Bandari ya
Mtwara ambayo ni ya tatu kwa ukubwa nchini baada ya Bandari ya Dar es Salaam na
Tanga umefanya jumla ya meli kubwa na za kisasa zilizotia nanga katika bandari
zetu nchini kufikia tatu.
Meli nyingine kubwa na ya kisasa kuja
nchini kwa mara ya kwanza ilikuwa ni Maersk Cubango mali ya Maersk Line iliyokuwa na
urefu wa mita 250
na upana wa mita 38 ikiwa na uwezo wa kubeba kontena 4,500.
Kabla ya ujio wa meli hiyo, Meli kubwa
nyingine ni MSC Martina yenye urefu wa mita 244 na upana wa mita 32.2 ikiwa na
uwezo wa kubeba makontena 2,411 pia ilifanikiwa kutia nanga katika Bandari ya
Dar es Salaam hivi karibuni.
Hii ni mara ya kwanza kabisa kwa Bandari ya Mtwara
kupokea meli kubwa yenye urefu wa mita 209 ikilinganishwa na meli ambayo
iliwahi kutia nanga katika Bandari ya Mtwara ambayo ilikuwa na urefu wa mita
205.
Meli hii kubwa iliingia Bandarini Mtwara tarehe
Februari 04, 2015 ikiwa na jumla ya Makontena 1,240 ambayo yalishushwa na
kupakia Makontena 1,027 yaliyosheheni Korosho.
Kitu pekee kilichokuwa kivutio wakati wa kuingia
kwa meli hiyo ni umaridadi wa Kapteni wa Bandari ya Mtwara Kapteni Hussein
Kasugulu kuingiza meli kwa kutumia ‘Tug’ moja tu ambapo ni vitu adimu kwa
Bandari nyingine kufanyika. Kwa kawaida meli huingizwa katika bandari kwa
kutumia ‘Tug’ mbili.
Meli hiyo inatarajiwa kuondoka Bandarini hapa
baada ya siku tano, ikishasheheni shehena ya mzigo wa korosho ambalo ni zao kuu
la biashara katika mikoa ya Kusini mwa Tanzania, haswa Mtwara.