HOTUBA YA MHESHIMIWA JAKAYA MRISHO KIKWETE, RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA WANAWAKE DUNIANI




YALIYOFANYIKA KITAIFA MKOANI MOROGORO
TAREHE 8 MACHI, 2015

Mheshimiwa Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto;
Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro;
Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri;
Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa;
Waheshimiwa Wabunge;
Mheshimiwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Morogoro na Viongozi Wengine wa Vyama vya Siasa na Mashirika ya Dini;
Waheshimiwa Viongozi na Watendaji wa Serikali;
Wageni Waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri Sophia Simba kwa kunialika na kunishirikisha katika sherehe za mwaka huu za Siku ya Wanawake Duniani.  Nakupongeza sana wewe na wenzako wote Wizarani na Mkoani Morogoro kwa maandalizi mazuri ya sherehe hizi.  Hakika mambo yamefana sana.   Niruhusuni pia nitoe shukrani maalumu kwa ndugu zetu wa Morogoro wakiongozwa na Mkuu wa Mkoa, Dkt. Rajabu Rutengwe kwa mapokezi mazuri na ukarimu wenu.  Vile vile nawapongeza kwa kukubali kubeba mzigo huu wa kuwa wenyeji wa sherehe hizi.  Natambua kuwa si kazi rahisi lakini mmeweza kufanikisha kwa kiwango cha hali ya juu sana.  Maonyesho ni mazuri na ukichanganya na jinsi wanawake walivyojitokeza kwa wingi tena wakiwa na nyuso zenye bashasha tele na kuvalia vizuri, kama ilivyo sifa ya wanawake wa Tanzania, hakika mmetia fora.  Mmezikonga nyoyo zetu kiasi cha kutufanya tutamani kuja tena Morogoro. Nawapeni pole kwa maafa yaliyotokea.  Nawapongeza kwa jinsi mlivyojijenga upya haraka.  Nitakuja kuwatembelea baadea ya sherehe.
Ndugu Wananchi;
Leo ni siku adhimu kwa wanawake wa Tanzania na wanawake wote duniani.  Ni siku yenu maalumu ya kuifurahia na kushangilia mafanikio mliyopata na kuweka msimamo kuhusu namna ya kukabili changamoto zilizowakabili sasa na zitakazojitokeza siku za usoni. Shamrashamra za akina mama waliojitokeza kwa wingi zinajieleza zenyewe kuwa leo ni siku ya furaha, siku ya kujipongeza na kusherehekea mafanikio ya wanawake wa Tanzania.  Hakika wanawake wa Tanzania wanayo kila sababu ya kusherehekea maana tumepiga hatua kubwa na ya kutia moyo katika jitihada za ukombozi na maendeleo ya mwanamke nchini. Kwa niaba yenu nawashukuru Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya Kimataifa kuja kujiunga nasi siku ya leo. 
Ndugu Wananchi;
Maadhimisho ya mwaka huu ya Siku ya Wanawake Duniani yana mambo mawili muhimu yanayoenda nayo sambamba.    Kwanza, kwamba huu ni mwaka wa 20 tangu kutolewa kwa Tamko la Beijing kuhusu Maendeleo ya Wanawake duniani.  Kama mjuavyo nchi yetu ilipata heshima katika mkutano ule wa 1995 pale Beijing kubwa kwa Mama Getrude Mongela kuwa Mwenyekiti wake.  Hivyo basi, maadhimisho ya mwaka huu ni fursa nzuri ya kufanya tathmini ya utekelezaji wa Tamko la Beijing miaka 20 baadae.
Pili kwamba, maadhimisho ya mwaka huu ni fursa ya kujadili namna nchi yetu itakavyojipanga kutekeleza uamuzi wa Umoja wa Afrika kuhusu uwezeshaji wa wanawake kimaendeleo kuelekea Ajenda ya Afrika ya mwaka 2063.  Katika mkutano uliopita wa Wakuu wa Nchi wanachama wa Umoja wa Afrika tuliazimia kuwa mwaka 2015 uwe ni wa kutoa msukumo maalum kuhusu Uwezeshaji wa Wanawake Kimaendeleo.  Waziri Sophia Simba alishiriki mkutano maalumu wa Mawaziri kuandaa agenda hiyo ya kikao cha Wakuu wa Nchi.  Nilimwambia pale Addis Ababa kuwa, atakaporudi aongoze katika kupanga mikakati na mipango ya kutekeleza azma hiyo ya Afrika hapa nchini.  Naamini kazi hiyo imeanza.  Bila ya shaka ndiyo maana basi kauli mbiu ya maadhimisho ya mwaka huu ni “Uwezeshaji Wanawake; Tekeleza, Wakati ni Sasa”. 
Utekelezaji wa Tamko la Beijing
Ndugu Wananchi;
          Kama nilivyokwishagusia awali, mwaka huu, Tanzania inajiunga na mataifa mengine duniani kuadhimisha miaka 20 ya utekelezaji wa Tamko la Beijing na Mpango Mkakati wa utekelezaji wa tamko hilo.  Tamko la Beijing lilisheheni mambo mengi yanayohusu haki,  hadhi na maendeleo ya mwanamke kwa lengo la kutoa fursa sawa kwa wanawake na kulinda utu wao dhidi ya dhuluma na ukandamizwaji wa mfumo dume. 
Mwaka huu, kila nchi inatakiwa kuwasilisha taarifa ya utekelezaji wake katika mkutano utakaofanyika tarehe 09 - 20 Machi, 2015 kule New York, Marekani. (59th Commission on the Status of Women Agenda Beijing +20)  Nafurahi kuwaarifu kuwa Tanzania itakwenda kwenye mkutano huo kifua mbele.  Tumetekeleza Tamko la Beijing kwa mafanikio makubwa hasa kuhusu  Uwezeshaji wa Wanawake Kiuchumi; Haki za Kisheria za Wanawake; Afya za Wanawake; na Usawa Katika Elimu, Mafunzo, Ajira na Nafasi za Uongozi na Uamuzi.  Ripoti ya nchi yetu iliyoandaliwa na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto ikishirikiana na wadau wengine imeyaeleza mafanikio haya kinagaubaga.  Bila ya shaka tumemsikia Waziri Sophia Simba akiyazungumzia baadhi ya mambo.  Nikuombe tu utafute wasaa mzuri uyafafanue vizuri kupitia vyombo vya habari ili watu wasikie.  Tuelezee yale tuliyofanikiwa na yale ambayo tunawajibika kuongeza nguvu na kasi zaidi.  Sema usikike vinginevyo unaacha ombwe la wasiotutakia mema kupotosha ukweli.



Uwezeshaji Kiuchumi
Ndugu Wananchi;
          Uwezeshaji wa wanawake kiuchumi ni jambo ambalo hapa Tanzania tumelipa kipaumbele cha juu.  Imekuwa hivyo kabla na baada ya Azimio la Ulingo wa Beijing.  Napenda kuanza kwa kutambua jitihada za makusudi za kuwawezesha wanawake kupata fursa za mikopo tulizofanya.  Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake (WDF) ulianzishwa kwa madhumuni hayo.  Hali kadhalika, Serikali ilihimiza kuanzishwa kwa Vyama vya Kuweka na Kukopa (SACCOS), VICOBA na asasi mbalimbali za micro-finance ambazo zimenufaisha wanawake wengi.  Hali kadhalika, Serikali imesaidia katika uanzishwaji wa Benki ya Wanawake Tanzania mwaka 2009. Benki ya Wanawake imepata mafanikio makubwa tokea kuanzishwa kweke.  Akaunti zimefikia 33,615, ina matawi mawili Dar es Salaam na vituo 81 vya mikopo na mafunzo Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Njombe, Ruvuma, Mara na Mwanza.  Kati ya Januari 2011 na Machi, 2014, Benki hii imetoa mikopo ya jumla ya shilingi bilioni 24,342,382,000 kwa watu 11,754 ambapo asilimia 88 ya watu hao ni wanawake.
  Aidha, Benki hii imewafikia wateja wanawake 19,000 kati ya mwaka 2009 na 2013.  Kwa Benki ya umri wa miaka mitano, huu ni mwanzo mzuri.  Sisi katika Serikali tutaendelea kuiwezesha benki hii kwa kuiongezea mtaji ili iweze kupanua shughuli zake na kuongeza matawi yake nchini.  Lengo letu ni kuiwezesha kuwafikia wanawake wengi kadri inavyowezekana.  Tunataka wanawake wajue kuwa Benki hii ni yao na ipo kwa ajili yao. Kwa jumla, hatua hizo zimewawezesha wanawake wengi kupata mikopo waliyoitumia kufanya shughuli za kuboresha mapato yao na hali zao za maisha yao na familia zao.
          Kwa hakika yapo mambo mengi yanayothibitisha kuwa tumepiga hatua ya kutia moyo katika uwezeshaji wa wanawake kiuchumi.  Upo ushahidi, kwamba, ushiriki wa wanawake katika sekta ya biashara ndogo na kati (SME) umeongezeka sana.  Katika ripoti ya Mapitio ya Sera ya Biashara za Kati na Ndogo ya mwaka 2013, kwa mfano, inaonyesha kuwa wanawake wanamiliki asilimia 64 ya biashara hizo nchini.  Nyingi zipo kwenye sekta isiyo rasmi.  Aidha, utafiti wa hali ya uchumi ya mwaka 2010 (THDS) unaonyesha kuwa asilimia 23 ya wanawake wana kipato kinachozidi au kulingana na waume zao.
 Wanawake wanaoshiriki kwenye maonyesho ya kibiashara wameongezeka kutoka 2,000 mwaka 2005 hadi 5,000 mwaka 2013.   Wakati mwingine huhitaji hata takwimu kujua ukweli huu.  Ukitembelea mabanda ya maonyesho ya bidhaa, maduka na masoko utaziona bidhaa nyingi za usindikaji zinazozalishwa na akina mama. 
Ndugu Wananchi;
Siku hizi akina mama wanaokwenda kununua bidhaa nje ya nchi hasa Dubai, China, Hong Kong, Bankok, Uturuki na kwingineko wamekuwa wengi sana.  Takwimu zinaonyesha kuwa kwa mwaka 2014 wanawake 2,243 walikwenda China kununua bidhaa mbalimbali.  Zamani haikuwa hivyo.  Hivi sasa wanawake siyo tu wanao uwezo wa kiuchumi bali pia hawana woga wa kusafiri masafa ya mbali.  Leo hii familia nyingi zinaendeshwa na akina mama wajasiriamali. Huu ni ukweli ulio wazi.  Sishangai kusikia kwamba baadhi ya wanaume wanaanza kutishika hata kusababisha kusikika kuwana mawazo ya kuanzisha vyama vya kutetea haki za wanaume. Kina mama kazeni buti, msirudi nyuma.  Mnafanikiwa.  Wanaume wanaolalama waacheni walalame.
Ndugu Wananchi;
          Hapana ubishi kuwa ukiwawezesha wanawake kiuchumi unaondoa umaskini katika familia.  Familia ambazo mama na baba wana kipato hali yao ya maisha ni bora zaidi.  Sisi Tanzania, asilimia 51 ya Watanzania ni wanawake.  Bahati mbaya sana kwa sababu ya mila zetu na hasa ukatili na uonevu wa mfumo dume unaotawala sasa, wanawake wanaongoza kwa idadi ya kuwa maskini.  Hivyo basi, kuwawezesha wanawake kiuchumi ndio ngazi ya kupandia katika kupunguza umaskini wa wananchi na nchi kupata maendeleo.  Ndiyo sababu, kwa upande wetu, Serikalini uwezeshaji wa wanaweke si jambo la kisera tu, bali ni la kimkakati na lipo kwenye mipango.  Katika kufikia shabaha za Dira ya Taifa ya Maendeleo kwa 2025 ya kuwa taifa la uchumi wa kati, nafasi ya wanawake imetambuliwa.  Ni sera ya msingi ya Serikali yetu kuendelea kuwawezesha wanawake hadi atakapokombolewa mwanamke wa mwisho kutoka kwenye lindi la umaskini. 
Ndugu Wananchi;
Naomba mtambue kuwa, tunapofanya hivi hatufanyi upendeleo kwa wanawake kwa ajili ya kujifurahisha wala kulipa fadhila, bali tunatimiza wajibu wetu wa msingi wa kutenda haki kwa kila raia.  Tunawarudishia wanawake haki yao na stahili yao, ambayo jamii iliwapokonya kwa muda mrefu.  Wanawake na wanaume ni sawa katika ubinadamu na utu wao.  Kwa ajili hiyo wanawake hawastahili kubaguliwa, kudhulumiwa na kufanyiwa uonevu na ukatili wa aina yo yote..
Haki za Kisheria za Wanawake
Ndugu Wananchi;
Tumepiga hatua kubwa kwa upande wa kuweka mazingira mazuri ya kisheria ya kulinda utu wa wanawake, heshima na fursa za kiuchumi na kijamii.  Tangu mwaka 1995, baada ya Tamko la Beijing, tumetunga Sheria nyingi zenye kuwapa haki wanawake dhidi ya mila na desturi potofu na zilizo kandamizi kwao.  Kwa mfano, mwaka 1998 tulitunga Sheria ya Makosa ya Kujamiiana (SOSPA) ambayo imeainisha adhabu kali ikiwemo kifungo cha miaka 30 kwa makosa ya ubakaji, kutembea na wanafunzi na udhalilishaji mwingine wa kijinsia.
Jambo lingine lililowekewa Sheria ni kuhusu wanawake kumiliki ardhi.  Sheria ya Ardhi Namba 4 na Sheria ya Ardhi ya Kijiji Namba 5 za mwaka 1999 zimeleta mapinduzi makubwa kwa kuwapa wanawake haki ya kumiliki ardhi.  Sheria ile ilifanyiwa marekebisho mwaka 2002 chini ya Sheria Na.2 kwa kuunda Mabaraza ya Ardhi ambayo lazima Wajumbe wasiopungua watatu, kati ya saba, wawe wanawake ili kuwapa sauti kwenye uamuzi uhusuo ardhi. 
Mwaka 2008 tukatunga Sheria nyingine mbili muhimu nazo ni ile ya Mikopo ya Nyumba (Mortgage Finance Special Provision Act) na ile ya umiliki wa kitalu au nyumba (Unit Titles Act).  Sheria hizi mbili zinasaidia kuwakinga wanawake dhidi ya dhuluma pale ambapo mume atauza ardhi au nyumba ambayo wamechuma pamoja bila idhini ya mkewe.
Ndugu Wananchi;
 Katika Katiba Inayopendekezwa haki ya wanawake kumiliki ardhi imetambuliwa rasmi na kuingizwa.  Hivyo basi, Katiba Inayopendekezwa ikipita itakuwa ni ukombozi wa aina yake kwa wanawake.  Aidha, imekomelea masuala mengine muhimu kwa haki za wanawake.  Miongoni mwayo ni lile suala la usawa katika vyombo vya uamuzi ambako sasa inapendekezwa kuwa Bungeni idadi ya Wabunge wanawake na wanaume iwe nusu kwa nusu (fifty fifty).  Masuala haya mawili na mengineyo ni muhimu kwa maslahi na maendeleo ya wanawake sasa yatakuwako kikatiba na sio tu kisheria pekee kama Katiba Inayopendekezwa itapita.
Ndugu Wananchi;
 Ni vyema kutambua pia kuwa haya yamewezekana kutokana na ushiriki mpana na mzuri wa wanawake kwenye mchakato wa Katiba unaotarajiwa kuhitimishwa kwa Kura ya Maoni mwezi ujao.  Katika Tume ya Marekebisho ya Katiba, wanawake walikuwa asilimia 30, na katika Bunge Maalumu la Katiba wanawake walikuwa 256 kati ya Wajumbe 620 wa Bunge hilo, yaani walikuwa asilimia 41.2.  Aidha, kulikuwa na mtandao wa Wanawake na Katiba uliohusisha asasi 110. 
Ombi langu kwenu akina mama, jitokezeni nyote mjiandikishe kupiga kura na siku hiyo ikifika muweze kuipigia kura ya NDIYO Katiba Inayopendekezwa.  Itakuwa Katiba mkombozi wa wanawake.  Itaondoa vikwazo vyote vikubwa kwa maendeleo na ustawi wa wanawake nchini.  Msikubali kuachwa nyuma mkapoteza fursa hii ya aina yake.



Afya kwa Wanawake
Ndugu Wananchi;
          Tumepiga hatua ya kutia moyo kwa upande wa haki ya wanawake kupata huduma ya afya katika miaka 20 ya uhai wa Tamko la Ulingo wa Beijing.  Ni ukweli ulio dhahiri kuwa hali ya afya ya wanawake ni bora zaidi leo kuliko ilivyokuwa miaka 20 iliyopita.  Ninyi ni mashahidi wa juhudi zetu za kupambana na mila potofu na hasi kama vile ukeketaji, ndoa za utotoni na mengineyo.  Mafanikio yameanza kuonekana.  Tumesimamia na kuhimiza sana kuhusu uzazi wa mpango ambao unatoa fursa kwa mwanamke kupanga uzazi wake. 
          Mageuzi makubwa katika huduma ya afya nchini yamejumuisha afya ya wanawake. Tumeyafanya hivyo kupitia Mpango wa Taifa wa Miaka Kumi wa Afya ya Msingi (MMAM 2007 – 2010) na Progamu kadhaa maalumu.  Kipaumbele cha juu kimetolewa kwa afya ya mama na mtoto.  Upanuzi mkubwa na uboreshaji wa huduma ya afya ya msingi pamoja na ya uzazi kusogezwa karibu na wanapoishi watu imesaidia sana kuboresha afya ya wanawake na watoto na kuokoa maisha yao.  Vituo vya afya na zahanati nyingi na mpya zimejengwa na kuboresha zilizopo.  Hiyo imeongeza na kuboresha huduma ya afya kwa wanawake vimejengwa na watoto.  Kwa ajili hiyo, vyumba vya kujifungulia kwa kina mama vilijengwa katika vituo vya afya na zahanati zilizokuwa hazina.  Kwa sababu ya umbali wa kwenda kujifungulia kupungua, idadi ya wanawake wanaojifungua katika mikono salama imeendelea kuongezeka na kufikia asilimia 51 mwaka 2014.  Ndiyo maana na vifo vya akina mama vinavyotokana na uzazi nchini vimeendelea kupungua.
  Mwaka 2005 wanawake 578 walifariki kwa kila uzazi salama 100,000 na kupungua hadi 432  mwaka 2012.  Juhudi zetu na matokeo haya yanawakilisha dhamira yetu ya kumfikia kila mwanamke na huduma hizi za afya mahsusi kwa wanawake.  Hata hivyo, bado ni vifo vingi mno, hatuna budi kuongeza bidii.  Tunataka hata mwanamke mmoja asipoteze maisha katika tendo la kumpa uhai mwanadamu mwingine.  Tutaendelea kuboresha huduma ya afya kwa wanawake ili hatimaye wanawake wote wanufaike na kunusurika na vifo vinavyoweza kuzuilika.
Wanawake Katika Uongozi na Ngazi ya Uamuzi
Ndugu Wananchi;
          Jambo ambalo hatujalifanyia ajizi ni kuwezesha wanawake kuingia kwenye uongozi na ngazi za uamuzi.  Tanzania ni mojawapo ya nchi 20 duniani na ya tano Afrika zenye Wabunge wanawake zaidi ya asilimia 30.  Sisi tunao Wabunge wanawake 126 kati ya 356 sawa na asilimia 36.  Kwa upande wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, wanawake ni 29 kati ya 80 sawa na asilimia 36.  Aidha, Spika wa Bunge letu ambaye ni kiongozi wa mmoja wa mhimili mkuu wa dola ni mwanamke, dada yantu Anna Semamba Makinda.  Kwa upande wa Mawaziri, idadi yao nao imekuwa ikiongezeka kutoka asilimia 15 mwaka 2004, asilimia 27 mwaka 2009, na asilimia 31 mwaka 2013. Hali kadhalika, kwa upande wa Majaji wa Rufani na Majaji wa Mahakama Kuu ambao idadi yao wote ni 97 kati yao 30 ni wanawake.  Hii ni sawa na asilimia 39.2.  Haya ni mageuzi makubwa sana katika Mahakama. 
Kwenye ushiriki wa wanawake katika nafasi za uamuzi tumefanikiwa sana hata kuliko baadhi ya mataifa makubwa.  Kwa mfano Uingereza wanawake ni asilimia 22 tu ya Wabunge wote katika Bunge la umri karne saba na nusu.
Ndugu Wananchi;
          Kutoa fursa na nafasi za uongozi na uamuzi kwa wanawake ni matokeo ya mkakati wa makusudi wa Serikali yetu kwa kutekeleza Sera za Chama Tawala.  Tumefanya hivyo kwenye Katiba, kwenye Sheria na hata Kanuni mbalimbali.  Hata katika utumishi wa umma kwa mfano, tumeleta mabadiliko makubwa kwa kuingiza kipingele cha 12(4) cha Kanuni za Utumishi wa Umma za 2013 kisemacho, “Inapotokea mwanamke na mwanaume wametimiza vigezo sawa kwa kulingana, basi kipaumbele atapewa mwanamke”.  Uamuzi kama huu wa kimapinduzi umesaidia sana kuongeza wingi wa wanawake katika ngazi mbalimbali za utumishi wa umma.  Nina matumaini kuwa katika Uchaguzi Mkuu mwaka huu wanawake wengi zaidi watajitokeza kugombea Udiwani, Uwakilishi, Ubunge na hata Urais.  Wapo wanawake wenye uwezo kwa nafasi hizo zote.  Msikubali kuachwa nyuma.  Msikubali kutishwa mkatishika.
Ndugu Wananchi;
          Tunapofanya tathmini hii leo, tunaridhika kuwa tumepiga hatua kubwa katika kuendeleza hali, utu na heshima ya mwanamke nchini.  Inatia moyo kuona kuwa hali hiyo inaonekana katika nyanja zote.  Jitihada zetu za kutoa fursa sawa kwa wote zinafanikiwa.  Leo hii, katika elimu ya msingi wasichana ni asilimia 50.6 na wavulana asilimia 49.41, katika elimu ya sekondari wavulana ni asilimia 52.1 na wasichana ni asilimia 47.9.  Ndio maana haishangazi kuwa katika wanafunzi 10 bora katika mtihani wa mwaka 2013 wa Sekodnari saba ni wanawake.  Katika VETA wasichana wameendelea kuongezeka na kufikia asilimia 38.5 na wavulana ni asilimia 61.5.  Katika vyuo vikuu wasichana sasa ni asilimia 34.6 na wavulana ni asilimia 65.4.  Tunaendeleza jitihada za kupanua fursa kwa wasichana katika vyuo vikuu na VETA ili tufikie nusu kwa nusu.
Hitimisho
Ndugu Wananchi;      
Kama mjuavyo, baada ya uchaguzi wa Oktoba, 2015, nitastaafu.  Kwa kweli, nitakwenda kupumzika kwa amani nikijivunia kutenda haki na kutoa fursa nyingi kwa wanawake nchini.  Ninaridhika kuwa nitaacha msingi imara wa haki za wanawake ambao naamini viongozi wetu wataofuatia watauendeleza zaidi kama mimi nilivyojenga juu ya msingi uliojengwa na viongozi walionitangulia. Mimi naamini wanawake wanaweza.  Naamini pia kuwa kuwekeza kwenye maendeleo ya wanawake ni kuwekeza kwenye mustakabali mwema kwa taifa.   Napenda kurudia kusema kuwa kuwapa fursa wanawake sio upendeleo, bali ni kuwapatia kilicho chao na kilicho haki yao.  Haya shime wote tuungane na kuwawezesha wanawake.  Aliwahi kusema Mwanafalsafa na mshairi Alphonse Lamartine katika karne ya 19, aliyepata kuishi kule Ufaransa, “kuna mwanamke mwanzoni mwa kila jambo jema na kubwa”.  (There is a women at the beginning of all great things).  Nami naamini kuwa nchi yetu itakuwa imeendelea pale tutakapompa kila mwanamke uhuru wa kujiendeleza.  Nguvu kubwa ya wanawake ambayo sasa haitoi mchango wake ipasavyo, itakapofanya hivyo nchi yetu itapaa
          Inawezekana, timiza wajibu wako.

Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania
Asanteni kwa kunisikiliza.

Post a Comment

Previous Post Next Post