Rais Kikwete aiomba India kugharamia ujenzi wa reli ya Dar es Salaam



THE UNITED REPUBLIC OF TANZANIA
DIRECTORATE OF PRESIDENTIAL COMMUNICATIONS
Telephone: 255-22-2114512, 2116898
Website : www.ikulu.go.tz              

Fax: 255-22-2113425


Description: Description: Description: Description: Description: Description: Coat of Arms
PRESIDENT’S OFFICE,
      STATE HOUSE,
              1 BARACK OBAMA ROAD,  
11400 DAR ES SALAAM.
Tanzania.
 
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Rais Kikwete aiomba India kugharamia ujenzi wa reli ya Dar es Salaam
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameiomba Serikali ya India kukubali kugharamia ujenzi wa reli  katika Jiji laDar es Salaam ili kupunguza misongamano mikubwa ya magari na kuongeza usafisi wa usafiri katika Jiji hilo.
Ombi hilo la Serikali ya Tanzania limetolewa na Rais Kikwete asubuhi ya leo, Ijumaa, Juni 19, 2015, wakati alipokutana kwa mazungumzo rasmi na Waziri Mkuu wa India, Mheshimiwa Narendra Modi, ikiwa ni sehemu ya shughuli za Rais Kikwete kwenye ziara yake rasmi ya Kiserikali ya siku nne katika India kwa mwaliko wa Rais wa nchi hiyo, Mheshimiwa Pranad Mukherjee.
Katika mazungumzo hayo, Rais Kikwete amemweleza Waziri Mkuu Modi kuhusu jinsi wingi wa magari ulivyoongeza misongamano mikubwa ya magari na hivyo kupunguza sana ufanisi wa usafiri kwa mamilioni ya wakazi wa Jiji hilo. Inakadiriwa kuwa Mji wa Dar Es Salaam una wakazi zaidi ya milioni nne kwa sasa.  
Katika maelezo yake, Rais Kikwete ameiomba Serikali ya Modi kufikiria uwezekano wa kugharamia ujenzi wa reli ya juu ya ardhi (siyo ya chini ya ardhi) kama njia ya uhakika zaidi ya kupunguza misongano.
Rais Kikwete amemwambia Waziri Mkuu kuwa tayari amezungumza na Kampuni ya Infrastructure Leasing and Financial Services (IFLS)  ya India ambayo imeonyesha hamu ya kushiriki katika ujenzi wa reli hiyo kwa nia ya kuongeza ufanisi wa usafiri kwa wakazi wa Dar es Salaam.
Jana, Alhamisi, Juni 18, 2015, miongoni mwa watu wengine, Rais Kikwete alifanya mazungumzo na Mwenyekiti wa ILFS, Bwana Ravi Parthasarathy kuhusu ujenzi wa reli hiyo na Mwenyekiti huyo akaonyesha hamu kubwa ya kufanya hivyo ili mradi Serikali ya India ishauriwe na kukubali kugharamia mradi huo.
 

wakati huo huo Serikali ya India imesema kuwa iko tayari kuongeza nafasi na fursa za raslimali fedha na nafasi kwa Tanzania katika maeneo mbalimbali yakiwemo  elimu, afya,  kilimo, ulinzi na mapambano dhidi ya ugaidi.
Aidha, Serikali ya India imesema kuwa itaanzisha utaratibu ambako Watanzania wanaoomba visa za kuingia India kwa ajili ya matibabu sasa wanaweza kuomba na kupata visa hizo kwa njia ya mtandao (e-visa).
Hatua hizo za Serikali ya India kwa Tanzania zimetangazwa leo, Ijumaa, Juni 19, 2015, wakati Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Mheshimiwa Narendra Modi alipokutana kwa mazungumzo rasmi ya Kiserikali na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ambaye yuko katika ziara rasmi ya siku nne nchini India kwa mwaliko wa Rais Pranab Mukherjee.
Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Hyderabad, Waziri Mkuu ambaye ndiye kiongozi wa Serikali katika India alisema kuwa Serikali yake iko tayari kupokea na kutafakari maombi mapya ya Tanzania katika maeneo ya ushirikiano wa kijeshi kama Tanzania inahitaji kuimarisha zaidi majeshi yake na shughuli za ulinzi katika dunia ya sasa iliyobadilika sana.
Amesema kuwa India iko tayari kupokea na kutafakari maombi ya ushirikiano wa pamoja katika maeneo ya usalama wa bahari hasa katika kukabiliana na tishio la ugaidi katika Bahari ya Hindi.
Waziri Mkuu pia amesema kuwa India iko tayari kuongeza nafasi za masomo kwa Tanzania na wanafunzi wake. Mpaka sasa, kiasi cha wanafunzi 2,000 wanasoma katika vyuo vikuu na taasisi nyingine za elimu ya juu katika India.
“Tuko tayari kuongeza nafasi za masomo na elimu na katika maeneo mengine ya ujenzi wa uwezo wa Watanzania,” amesema Waziri huyo.
Kuhusu upatikanaji wa visa kwa Watanzania ambao wanataka kuingia katika India kwa ajili ya kupata  matibabu, Mheshimiwa Modi amesema kuwa India imekubali kuwa Watanzania wanaotaka huduma za tiba, wataweza kuomba visa kwa kutumia njia ya mitandao na hivyo kupata visa haraka zaidi kuliko sasa.
Mara baada ya mazungumzo hayo, viongozi hao wawili wamehudhuria mkutano na waandishi wa habari ambako wameshuhudia utiaji saini mikataba minane ya ushirikiano kati ya Tanzania na India.
Mapema leo asubuhi, Rais Kikwete alipokelewa rasmi na Rais Mukherjee katika sherehe zilizofanyika kwenye Ikulu ya India ya Rashtrapati Bhavan, sherehe ambayo pia imehudhuriwa na Waziri Mkuu Modi.
Rais Kikwete amepigiwa mizinga 12 na kukagua gwaride kwa heshima yake katika sherehe hiyo iliyochukua kiasi cha dakika 10. Baada ya sherehe hiyo, Rais Kikwete ametembelea Jumba la Kumbukumbu Mahatma Gandhi la Rajghat lililoko mjini New Delhi.
Rais Kikwete pia amekutana kwa mazungumzo na Waziri wa Mambo ya Nje wa India, Mheshimiwa Sashma Swaraj katika mazungumzo yaliyofanyika kwenye Hoteli ya Taj Palace ambako Rais Kikwete na ujumbe wake amefikia.
Rais Kikwete pia amekutana na kufanya mazungumzo na Makamu wa Rais wa India, Mheshimiwa Mohammad  Hamid Ansari na Waziri wa Afya na Ustawi wa Familia, Mheshimiwa J.P Nadda.
Baadaye  jioni, Rais Kikwete alitarajiwa kuhudhuria dhifa ya kitaifa iliyokuwa inaandaliwa kwa heshima yake na Rais Mukherjee.
Imetolewa na;
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu – Dar es Salaam.
19 Juni, 2015

Post a Comment

Previous Post Next Post