MATOKEO YA UBUNGE MBAGALA YAPINGWA NA UKAWA



WAGOMBEA  wa vyama tofauti waliokuwa wanagombea ubunge   Mbagala wameungana kupinga matokeo yaliyobandikwa katika Kituo cha Shule ya Msingi Majimatitu ambayo yamempa ushindi mgombea wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Issa Mangungu.
Wagombea hao wanaotoka katika chama Cha Wananchi (CUF), ACT- Wazalendo, AFP, NCCR-Mageuzi, wanayapinga matokeo hayo wakidai si ya halali.
Matokeo yaliyobandikwa katika kituo hicho na kugongwa muhuri wa Mkurugenzi yanaonyesha mgombea wa CCM, Mangungu ameshinda kwa kura 87,249 akifuatiwa na wa CUF , Kondo Bungo aliyepata kura 77,043.
Akizungumza na waandishi wa habari jana katika ofisi za chama hicho, Temeke  Dar es Salaam, Bungo alisema matokeo hayo yamepikwa na ni kinyume na sheria.
"Tunayakataa kwa sababu katika.makubalino yetu.juzi na.mkurugenzi wa Temeke, Photidas Kagimbo, tulikubaliana uchaguzi umeharibika na ilikuwa jana atoe tamko lakini hata uhakiki bado haujafanyika.
“Juzi tulibaini kasoro nyingi ikiwamo kasoro ambayo Kata ya Kijichi ilionyesha nimepata kata moja wakati karatasi za wakala zinaonyesha nimepata kura 78  na kuna kata ilikuwa na vituo 94 lakini walileta matokeo ya vituo 80 na mkurugenzi alikiri kasoro hizo...tunashangaa jana wamebandika na yana muhuri wa mkurugenzi,” alisema Kondo.
Alisema wameamua kufanya mazungumzo na wanasheria wao  kuweza kutoa uamuzi wa pamoja kuhusiana na matokeo hayo.
Kondo alisema anachoweza kusema ni kuwa wananchi wa Mbagala wafahamu haki yao imepokwa na wao binafsi kila mmoja atajua jinsi ya kudai haki yake.
“Wananchi watafakari kila.mmoja dhuluma hii na kila.mtu atajua hatua za kuchukua,” alisema Kondo.
Vyama vingine vilivyogombea ni   TADEA kilichopata kura 607, AFP 739, CHAUSTA 362, Demokrasia Makini  264, NRA 238  na NCCR Mageuzi 2,156.
Waandishi wa gazeti hili walitembelea  kituo hicho cha shule ya Majimatitu na kukuta ulinzi ukiwa umeimarishwa na baadhi ya maduka yakiwa yamefunguliwa.
MTANZANIA ilifanya jitihada za kumtafuta mkurugenzi Magimbo   kupata ufafanuzi zaidi wa matokeo hayo lakini  simu yake ilikuwa haipatikani na pia hakuwapo ofisini.

Post a Comment

Previous Post Next Post