KAMANDA wa Polisi Kanda Maalum ya
Dar es Salaam, Naibu Kamishna Simoni Sirro, ameahidi zawadi ya Sh milioni moja
kwa atakayetoa siri ya jambazi anayetumia bunduki aina ya SMG kwani silaha hiyo
ni hatari.
Kamanda Sirro alitoa kauli hiyo
jijini Dar es Salaam jana, wakati akizungumza na wakazi wa mtaa wa Nyambwera
kata ya Tandika Manispaa yaTemeke katika mkutano wa uhamasishaji ulinzi
shirikishi mtaani hapo.
Alisema kuwa silaha hiyo ni kubwa
hivyo yupo tayari kutoa fedha hizo kwa yeyote atakayefichua siri za kuwepo kwa
aina hiyo ya silaha.
Pia aliwataka vijana wa mtaa huo
kuachana na mambo ya uhalifu kwasababu uhalifu una mwisho wake na
kuwataka wazazi kuwaonya watoto wao wanaofanya biashara za kihalifu
na kuwakemea waache mara moja.
“Hakuna mtu anayepata heshima
kwaajili ya kazi ya wizi au ujambazi wakati kila mtu anajua mwisho wa wizi ni
nini kitachotokea, ni vyema kufanya biashara itakayokupatia kipato halali,”
alisema.
Kamanda Sirro ametoa onyo kwa
majambazi kuacha mara moja kazi hiyo na kama hawataki wataishia
mikononi mwake au kwa vijana wake.
Pia amewataka wananchi kutoa
ushirikiano kwa polisi ili kuwafichua majambazi, vibaka, wauza gongo na madawa
ya kulevya ili mtaa huo waishi kwa amani.
Kamanda Sirro pia aliwataka
wenyeviti wa mtaa kutimiza wajibu wao na kuhakikisha wananchi wanaishi
kwa amani kwani hiyo ni moja ya kazi yao.
Pia aliwataka wananchi kutoa taarifa
endapo wataona kuwa mwenyekiti hatimizi wajibu wao ili waweze kuwachukulia
hatua za kisheria kwa ni sasa hivi hapa ni kazi tu.