ASANTENI kwa kuja. Ndio ujumbe rahisi na wa dharau
ambao klabu ya Yanga imeutuma kwa wapinzani wao wakubwa, Simba, siku chache
baada ya kuwafunga mabao 2-0 katika mchezo mkali wa Ligi Kuu ya Vodacom
Tanzania Bara, uliochezwa katika Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam mwisho
wa wiki iliyopita.
Picha kamili liko hivi: Matokeo ya juzi yalimaanisha
kuwa Yanga imeshinda mechi zake zote mbili dhidi ya Simba msimu huu na katika
mapambano yote hayo walishinda kwa mabao 2-0, kitu ambacho tayari kimeanza
kuwapa jeuri na kujiona wao ni levo nyingine.
Na hiki ndicho kimewafanya sasa wadiriki kusema kuwa
Simba si levo yao tena na watabaki kuwa watani wao wa jadi tu, lakini si
wapinzani wao wakubwa kwa sababu viwango vyao ni tofauti kama mbingu na ardhi.
Yanga, ambayo ushindi wake ulitokana na mabao ya
mastraika wake wa kimataifa, Donald Ngoma (Zimbabwe) na Amis Tambwe (Burundi),
wametoa kauli hizo za dharau dhidi ya Simba kupitia kwa Mkurugenzi wake wa
Mawasiliano, Jerry Muro.
Muro aliliambia BINGWA kuwa wameamua kuvunja rasmi
upinzani wao dhidi ya Simba kwa sababu Wekundu hao wa Msimbazi si saizi yao
tena na sasa hivi wanahitaji timu nyingine ambayo itawapa upinzani wa kweli
ambao Simba wameshindwa kuutoa kwao.
“Tunatangaza rasmi kuvunja upinzani wetu na Simba
kutokana na ukweli kuwa sasa hivi hawa jamaa si saizi yetu,” alisema Muro. “Sisi
wa kimataifa na saizi yetu lazima wawe wa kimataifa pia, hawa Simba hawana
ladha tena, watabaki kuwa watani wetu tu, lakini kamwe hawawezi kuwa wapinzani
au washindani wetu kwa sababu si levo yetu.”
Muro aliendelea kutamba kuwa kitendo cha Yanga
kuipiga Simba kwenye mechi mbili mfululizo za Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu
kimethibitisha kuwa miamba hiyo ya Msimbazi si saizi yao tena.
“Kilichobaki sasa hivi tukutane nao kwenye mabonanza
ya mchangani, lakini kama kwenye ligi tumemalizana nao au kama kutakuwa na
mzunguko wa tatu tupo tayari pia kucheza nao, nasisitiza tena Simba si saizi
yetu,” alitamba Muro.
@@@@@