HAKUNA MGOMO WA MADAKTARI MASWA-DED

Na Benedict John-MAELEZO-Dar es salaam.
………………………………………………..
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Simiyu Trasias Kagenzi amekanusha madai yaliyoandikwa na baadhi ya vyombo vya Habari kuhusiana na taarifa za kufanyika kwa mgomo unaotarajiwa kufanywa na baadhi ya Madaktari na Wauguzi katika Hospitali mkoani Simiyu na kusema habari hizo sio za kweli.
Kauli hiyo ameitoa leo katika mahoajiano na Mwandishi wa Habari hii juu ya kuwepo kwa mgomo huo  ambapo alifafanua kuwa, taarifa hiyo haina ukweli wowote kwani siku ya tarehe 02 Februari mwaka huu, alikuwa na kikao na watumishi wote wa Hospitali hiyo ambapo kati ya mambo walioyajadili ni stahili na hali ya kazi hospitalini hapo.
”Hapa wilayani kwetu kuna baadhi ya waandishi ambao hawazingatii maadili ya kazi zao hasa kwa kuandika habari zisizo na ukweli, nimeshangaa kusikia taarifa hii kwasababu ukweli ni kwamba mimi nilikaa na watumishi wote jana wakiwemo madaktari, wauguzi na madereva na moja ya mambo tuliyojadili ni pamoja na mishahara yao na posho zao, na tulimaliza kikao chetu kwa amani kabisa, sasa waandishi kama hawa tunawaita makanjanja maana haina ukweli wowote”, alisema Kagenzi.
Aliongeza kuwa, kitendo walichokifanya baadhi ya waandishi hao kuandika habari hiyo sio jambo la busara kwani linaleta mkanganyiko na chuki baina ya watumishi na viongozi wao na hata kwa serikali yao na amelaani jinsi waandishi hao wanavyotumia kalamu zao vibaya kwa kupotosha umma wa watanzania
”Inasikitisha kwa kweli mtu anakurupuka bila kuwasiliana na Utendaji Mkuu wa Hospitali na kuanza kuanza kukutana na madaktari anaowajua na kuanza kuandika taarifa kama hizi na kuzirusha katika vyombo vya habari”, alisisitiza Kagenzi.
Mkurugenzi huyo amewataka waandishi wa habari kuzingatia maadili ya kazi zao ili waweze kuandika habari ambazo zinatoa picha halisi badala ya kuwaogopesha wananchi na hivyo kushindwa kwenda kupata huduma.
Kwa upande wake Afisa Habari wa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, Bi.  Stella  Kalinga alieleza kuwa baada ya kufuatailia taarifa aligundua kuwa siyo za kweli kwani hakuna dalili yoyote ya mgomo kwa watumishi hao wa afya na wako kazini wakiendelea na majukumu yao kama kawaida.

Post a Comment

Previous Post Next Post