MKALI wa nyimbo za injili nchini, George Kayala amekamilisha
albamu yake ya pili aliyoipa jina la Maajabu ya Damu ya Yesu ikiwa katika mfumo
wa CD ikiwa na nyimbo saba ambazo amedai zina nguvu ya ajabu na zitafanyika
msaada kwa kila atakayezisikiliza.
Akizungumza na mtandano huu leo, Kayala alisema kwamba hii
ni albamu ya pili baada ya ile ya kwanza iliyojulikana kwa jina la Siwema na
amewataka mashabiki wake kujiandaa kupata nakala halisi na si kununua feki.
“Nimekamilisha albamu ya pili itwayo Maajabu ya Damu ya Yesu
ikiwa katika mfumo wa CD ikiwa na nyimbo saba ambazo ni Maajabu ya Damu ya
Yesu, Kanitendea Mema, Fungua Njia, Dhihirisha Uwaza Wako, Wastahili Sifa, Umenikumbuka
na Tanzania,” alisema Kayala.
Mwimbaji huyo alisema kwa sasa anafanya maandalizi ya
kurekodi video yake na huenda zoezi likaanza mwishoni mwa mwezi huu ama
mwanzoni mwa mwezi wa tatu huku akiwataka wapenzi wote wa muziki kumuunga mkono
kwa kununua kazi zake ili apate fedha ya kurekodia video hiyo.