Mayanja acharuka Simba




KOCHA wa Simba, Jackson Mayanja, ameamua kuwafungia kazi wachezaji wake wote `waliopangwa` katika mchezo wa Jumamosi wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara na kukubali kichapo cha mabao 2-0 kutoka kwa watani wao wa jadi, Yanga.
Katika mchezo huo, Simba walianza kwa kasi, huku viungo wao wakigongeana vyema kabla ya kusambaratika baada ya kutolewa kwa kadi nyekundu beki wa kati wa timu hiyo, Abdi Banda, baada ya kumfanyia madhambi straika wa Yanga, Donald Ngoma.
Hali hiyo ilimlazimu Mayanja kumshusha kiungo Justice Majabvi kusaidiana na Jjuuko Murushid, hivyo kupunguza kasi katika ya safu yake ya viungo.
Mayanja ameliambia JIJILETU BLOG jijini jana, kwamba atakutana leo na wachezaji wake katika mazoezi, kikubwa ni kuwaweka sawa kisaikolojia pamoja na kufanyia kazi mapungufu na makosa yaliyojitokeza katika mchezo uliopita.
Alisema ameshangazwa na kiwango cha chini kilichoonyeshwa na wachezaji wake, hivyo anahitaji umakini wa hali ya juu katika kuhakikisha katika mazoezi yao ya leo anaangalia kila idara na kuwapiga msasa wachezaji wake.
 “Sijaelewa kwanini vijana wangu wamecheza chini ya kiwango bila ya kutarajia, lakini kwa kupoteza mechi hiyo hakumaanishi kuwa ndio tumekata tamaa katika mbio za ubingwa kwa kikosi changu,” alisema.
Mayanja alisema katika mazoezi yao atafanyia kazi safu yake ya ulinzi, viungo, hasa katika sekta muhimu ya ushambuliaji, ambayo haikuonyesha uhai wala madhara yoyote kwa wapinzani wao.
“Bado nina imani kubwa na vijana wangu, sasa jambo lililobaki ni kukaa na vijana nizungumze nao na kuangalia wapi natakiwa tufanyie kazi, pia suala la ubingwa naona bado sijapoteza matumaini kulingana na jinsi  tulivyopishana pointi,” alisema.
Mayanja alisema katika hatua hiyo ana imani bado ndoto zake za kuibuka na ubingwa zinaendelea, akiamini vijana wake watafanya vizuri katika michezo iliyobakia ya mzunguko wa pili wa Ligi hiyo.

Post a Comment

Previous Post Next Post