Mo ampa Ridhiwan milioni 100/-



TAASISI isiyokuwa ya kiserikali ya Mo Dewji, imemkabidhi Mbunge wa Chalinze, Ridhiwan Kikwete hundi ya Sh milioni 100 kwa ajili ya mradi wa ufugaji kuku wa kienyeji kwa wajasiriamali wa Kijiji cha Msoga, Chalinze mkoani Pwani.
Ofisa Uhusiano wa taasisi ya Mo Dewji, Zainul Mzige, alisema wametoa fedha hizo kama sehemu ya kurejesha faida kwa wananchi.
"Taasisi ya Mo Dewji inaendelea kufanya kazi katika miradi mingi ya maendeleo ya wananchi na imepania kujiingiza zaidi kwa namna bora ya kusaidia miradi yenye lengo la kutoa huduma itakayomuwezesha kila mwananchi kuwa na uwezo wa kujiendeleza na kustawi kiuchumi," alisema.
Alisema katika kufanikisha uwezeshaji huo, Taasisi hiyo imetumia zaidi ya dola milioni tatu kwa kipindi cha miaka mitano kuwezesha miradi mbalimbali ya maendeleo.
Kwa upande wake mratibu wa mradi huo, Novatus Karembo, alisema utanufaisha wananchi 722 katika vitongoji tisa wa Kijiji cha Msoga.
"Wazo la mradi huu lilibuniwa mwaka 2013 na Rais mstaafu Jakaya Kikwete,  tumeshaunda kikundi cha wanachama 241 kwa ajili ya utekelezaji wa awamu ya kwanza wa mradi huu," alisema.
Naye Ridhiwan Kikwete aliushukuru uongozi wa Mo Dewji kwa msaada huo.         
"Ijumaa nitakabidhi rasmi fedha taslimu kwa ajili ya kuanza mradi huo kwa sababu tumedhamiria kuwawezesha kiuchumi wananchi wetu...  huu ni mwanzo bado kuna miradi mingine mingi," alisema.

Post a Comment

Previous Post Next Post