Na Veronica Romwald, Dar es Salaam
WASICHANA wengi nchini wamekuwa wakiyaona masomo ya sayansi
kuwa ni magumu na mzigo mkubwa kwao hali inayotoa nafasi kwa wavulana kuchangamkia
masomo hayo ambayo yanatajwa kuwa na fursa nyingi za kiuchumi.
Tumesikia matamko mbalimbali ya viongozi wa ngazi za juu wa
serikali wakiwahimiza wasichana kuachana na mtizamo huo hasi kwa kuanza kuyapenda
na kujifunza masomo ya sayansi ili nao waje kuwa wataalamu wa fani tofauti
tofauti hapo baadae.
Necta Richard ambaye ni mwanafunzi wa kidato cha pili
katika Shule ya Sekondari ya Jangwani ni miongoni mwa wasichana walioamua
kuitikia wito huo wa kusoma masomo ya sayansi.
Anasema amejipanga kuhakikisha kuwa anafikia ndoto yake ya
kuwa Injinia mkubwa wa baadae nchini pindi Mungu atakapomuwezesha kuhitimu
masomo yake.
MTANZANIA lilipata fursa ya kuzungumza na Necta punde baada
ya kumaliza kuwasilisha hotuba mbele ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu wakati wa maadhimisho ya Siku ya Idadi ya
Watu Duniani Julai 11, mwaka huu kwa niaba ya wanafunzi wenzake 150.
Akizungumza, Necta anasema tangu akiwa mdogo amekuwa akitamani
kuja kuwa injinia, na kwamba alipoanza kusoma aliweka juhudi katika kujifunza
masomo ya sayansi ili kufikia ndoto yake hiyo.
Anasema kwa kuwa aliyapenda masomo hayo kila siku amekuwa
akijifunza kwa bidii na kuwasikiliza kwa makini walimu wake ili aweze kupata
uelewa mpana zaidi.
“Nataka kuwa injinia mkubwa ili kuisaidia nchi yangu,
nimepanga kusoma fani ya ‘Mechatronics’. Hii ni fani inayojumuisha mambo mawili
kwa pamoja yaani ‘Mechanical’ na ‘Enginearing’ ambapo nitaweza kupata ujuzi wa
vitu vingi kwa wakati mmoja kupitia fani hiyo, nitaweza kujua namna ya kutengeneza
magari, kuwa injinia wa masuala ya umeme, kutengeneza vyuma na vitu mbalimbali
vya aina hizo,” anasema.
Necta anasema wasichana wanapaswa kuachana na uwoga wa
kusoma masomo ya sayansi kwa sababu kuna fursa nyingi za kujikomboa kichumi katika
maisha yao ya baadae.
“Sijui kwanini wanaogopa na kuyakimbia masomo ya sayansi, lakini
hakuna jambo gumu kikubwa ni kuwekeza katika kujifunza ili kujijengea msingi
mzuri wa baadae kwa sababu masomo haya usipoweka msingi hapa awali huko mbele
lazima utayaona magumu kwako.
“Nimeambiwa wasichana wengi wanaikimbia fani hii ya ‘Mechatronics’,
ndio maana wanaofanikiwa kumaliza ni wanaume peke yao, mimi nataka nivunje
rekodi hiyo ya kuwa msichana wa kwanza kusoma fani hiyo,” anasema kwa
kujiamini.
Anasema anataka kuvunja rekodi hiyo na kuwa msichana wa
kwanza kusoma fani hiyo kwani licha ya wavulana kuisoma hata hivyo bado kuna
wataalamu wachache nchini.
“Kwa msingi huo utaona namna ambavyo fani hii ina fursa
nyingi za ajira. Nawashauri wasichana wenzangu wasiyakimbie masomo ya sayansi
bali wayapende na kutia juhudi ya kujifunza ili waje kujikomboa kiuchumi hapo
baadae,” Anasema.
Pamoja na hayo, Necta anasema wazazi wana jukumu kubwa la
kuhakikisha wanawasaidia watoto wao hasa wa kike katika kukabiliana na changamoto
mbalimabali wanazokumbana nazo kila siku.
“Mtoto wa kike anakabiliwa na changamoto nyingi kuliko
mtoto wa kiume na hili lipo wazi, kwa mfano kuna suala la unyanyasaji wa
kijinsia, ukeketaji, ndoa na mimba za utotoni ambazo kiukweli imekuwa ikiwafanya
wengi washindwe kutimiza ndoto zao.
“Hivyo wazazi wana jukumu kubwa la kuhakikisha wana walinda
watoto wa kike dhidi ya unyanyasaji wa kila aina ili wafikie malengo yao kama
ilivyo kwa watoto wa kiume, serikali nayo inapaswa iweke mazingira rafiki kwa
watoto wa kike na kuweka sheria za kuwalinda,” anasema.
Anasema serikali inapaswa kukomesha na kuziondoa kabisa
mila potofu dhidi ya mtoto wa kike ambazo zimekuwa zikikandamiza haki zao za
msingi pamoja na sheria zinazokandamiza haki zao.
“Kwa mfano ile sheria ya ndoa ni vyema wakiifanyia
marekebisho kwamba mtoto aolewe angalau akifikisha miaka 18 na si 14 kama
ambavyo inasema hivi sasa,” anasema.
Necta anasema anaishukuru serikali na Shirika la Umoja wa
Mataifa la Idadi ya Watu (UNFPA) kwa kuwezesha ziara ambayo yeye na wenzake 150
waliifanya kwa kuzunguka katika maeneo mbalimbali kujionea shughuli za
kiuchumi.
“Tuliweza kutembelea Hospitali ya Taifa Muhimbili, Chuo
Kikuu cha Sayansi na Tiba Muhimbili (MUHAS), kikundi cha kina mama
wajasiriamali Kimara ambako kwa kweli tulijifunza vitu vingi vya kitaaluma na
kiuchumi ambavyo vilitufungua ufahamu wetu.
"Nawashauri
wasichana wenzangu waje wajiunge na katika 'organization yetu ya apps'
ambapo watajifunza jinsi ya kutengeneza application mbalimbali ikiwamo
website hasa wale walio na umri wa miaka 13 hadi 18 ofisi zetu zipo
Kisutu Sekondari au wanipigie kwa namba 0787 106 744,” anasema.