MASHIRIKA yasiyo ya kiserikali (NGOs) ambayo yatabainika kuwa yanaendelea na miradi ya kusambaza vilainishi kwa wanaume wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja nchini yatafutiwa usajili wake.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,
Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu (Pichani) aliandika hivyo kupitia ukurasa wake wa mtandao
wa ‘facebook’ na kusisitiza kuwa serikali italisimamia kikamilifu suala hilo.
“Sijapiga marufuku matumizi ya vilainishi. Ukweli, Nimepiga
marufuku mashirika yasiyo ya kiserikali (NGOs) kununua na kusambaza vilainishi
kwa wanaume wanaojihusisha na mapenzi na wanaume wenzao. Sababu nimeshazieleza,”
aliandika.
Aliongeza “Na nafurahi kuwajulisha kuwa tayari
baadhi ya Mashirika hayo yameanza kutekeleza agizo hili kwa kuanza kuondoa
vilainishi kwenye miradi yao. Nayapongeza sana. Niendelee kuyataka mashirika
mengine kutii agizo hili ambalo tutalisimamia kikamilifu.
“Serikali haitasita kuchukua hatua ikiwemo
kuyafutia usajili mashirika yanayoendelea na miradi ya kusambaza vilainishi kwa
wanaume wanaojihusisha na mapenzi ya jinsia moja,” alisisitiza.
Aliyataka mashirika hayo kushirikiana na serikali kupambana na maambukizi ya virusi vya Ukimwi kwa kujikita kwenye afua nyingine zinazozingatia sheria za nchi sambamba na mila na desturi zetu watanzania.
Akizungumza Dar es Salaam hivi karibuni, Waziri
Ummy alisema serikali imechukua uamuzi huo kwani matumizi ya vilainishi hivyo yanachochea
kuongezeka kwa vitendo vya ushoga ambavyo ni kinyume cha sheria za nchi.
“Lengo pia ni kudhibiti maambukizi ya VVU kwa
sababu katika wanaume wanaojihusisha na
mapenzi ya jinsia moja, asilimia 23 tayari wana maambukizi hayo.
“Tumebaini baadhi ya wadau wanaotekelezeka
shughuli za makundi maalum wamekuwa wakikiuka taratibu za utendaji na kusambaza vilanishi hivyo. Katika
nchi yetu hakuna sheria inayoruhusu
uhusiano wa jinsia moja na kuendelea kusambaza vilainishi hivyo ni kama
kuhalalisha vitendo hivyo. Mila na desturi zetu haziruhusu uhusiano huo,”
alisema.