Na
Jacquiline Mrisho – MAELEZO
Halmashauri
ya Manispaa ya Ilala Jijini Dar es Salaaam
imewataka wafanyabiashara kuzingatia muda uliopangwa na Serikali kwa ajili
ya usafi wa mazingira katika maeneo yao ya kazi unaofanywa kila ifikapo siku ya
jumamosi.
Muda
uliowekwa kwa ajili ya zoezi hilo ni kuanzia saa 12:00 asubuhi hadi saa 3:30
asubuhi, ambapo wafanyabiashara wote watapaswa kufungua maduka na masoko yao mara
baada ya zoezi hilo kukamilika.
Hayo
yamesemwa leo na Afisa wa Manispaa hiyo, David Langa wakati alipokuwa akiongea
na mwandishi wa habari hii kuhusu mwitikio wa wananchi juu ya zoezi la usafi wa
mazingira unaofanyika kila jumamosi na kila mwisho wa mwezi.
“Nawaomba
Wafanyabiashara wenye tabia ya kujichelewesha ili wafike baada ya muda wa usafi
pamoja na wale wanaofungua biashara kabla ya muda uliopangwa na Serikali kuacha
mara moja kwani lengo la kubadili muda
wa kufungua biashara ni kwa ajili ya kufanya usafi” alisema Langa.
Akifafanua
zaidi Langa aliwatahadharisha wananchi wanaopenda kutupa taka hovyo kuacha mara
moja kwani sheria ya afya na sheria ya mazingira inapinga suala hilo na kwa
mujibu wa sheria hizo adhabu yake ni faini ya shilingi milioni moja au kifungo
kisichozidi miaka 6.
Kwa
mujibu wa Langa alisema kuwa, suala la usafi sio suala la Serikali pekee bali
wananchi wanatakiwa walifanye kuwa ni sehemu ya kulinda afya zao, hivyo kila
mmoja anapaswa kuzingatia usafi kwenye maeneo yanayomzunguka.
Aidha
Langa alisema kila mwananchi anapaswa kuwa mlinzi wa mwenzie kwani zoezi la kulipishwa
faini bado ni endelevu, mtu atakaemkamata mwenzie anatupa taka atapewa shilingi
elfu 20 na aliyekamatwa atatoa faini ya shilingi elfu 70.
MWISHO