Shirikisho la
Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limetangaza kiingilio cha Sh 2,000 kwa mzunguko
na Sh 5,000 kwa jukwaa kuu wakati timu ya taifa ya Tanzania ya vijana wenye
umri wa chini ya miaka 17 itakapocheza na Amajimbos ya Afrika Kusini kwenye
mchezo wa kuwania nafasi ya kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika zitakazofanyika Madagascar, mwakani.
Serengeti Boys |
Jumamosi Agosti
6, 2016, Serengeti ilitoka sare ya 1-1 na Afrika Kusini katika mchezo uliofanyika
Uwanja wa Dobsonville ulioko Soweto, Mji ulioko Kusini – Magharibi mwa jiji la
Johannesburg, mabao yote yalipatikana kipindi cha pili yakiwa ni ya penalti kwa
kila upande. Afrika Kusini ndio walioanza kupata penalti katika dakika 65
iliyofungwa na Luke Gareth kabla ya Ally Msengi kuisawazishia Serengeti Boys katika
dakika ya 70.
Penalti ya
Afrika Kusini ilitokana na mmoja wa mabeki wa Serengeti Boys kumfanyia madhambi
Linamandla Mchilizeli wa Amajimbos ndani ya eneo la hatari wakati ile ya
Serengeti Boys ilitoakana na beki Luke Donn wa Amajimbos kunawa mpira eneo la
hatari. Mwamuzi wa mchezo huo alikuwa, William Koto kutoka Lesotho.
Kocha Mkuu wa Serengeti
Boys, Bakari Shime maarufu kama Mchawi Mweusi amesema: “Watanzania wakaribie
Chamazi, waje kutushangilia ili tushangilie ushindi kwa pamoja kikosi change kiko
vema na ninamshukuru Mungu kwa hilo, akili yangu na akili za wachezaji wangu ni
kumuondoa Msauzi (Afrika Kusini).”