Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Paul Makonda amewataka watendaji
wa mkoa huo kuhakikisha kuwa wanasimamia ubora wa madawati
yanayotengenezwa na vyumba vya madarasa vinavyojengwa maeneo mbalimbali
ya mkoa huo.
Aidha, amezitaka manispaa za mkoa huo kuendelea kutenga fedha kwa
ajili ya kujenga madarasa mapya na kuwahamasisha wananchi na wadau
mbalimbali wa maendeleo kujitolea kufanikisha mpango huo na kutoa wito
kwa madiwani kujiwekea mkakati wa kujenga walau madarasa mawili kwenye
Kata zao.
RC Paul Makonda |
Akifungua kikao chake cha kwanza cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Dar
es salaam (RCC), Mhe Makonda amesema kuwa licha jiji hilo kukabiliwa na
changamoto za kimaendeleo za muda mrefu kwenye sekta ya elimu,
miundombinu ya Afya, maji na barabara mafanikio yameanza kuonekana
kutokana na juhudi za pamoja za viongozi wa mkoa huo.
UPATIKANAJI WA MADAWATI
Kuhusu upatikanaji wa madawati amesema kuwa toka Mhe. Rais wa Jamhuri
ya Tanzania atangaze kampeni ya upatikanaji wa madawati kwa ajili ya
shule za Msingi kumekuwa na mwitikio mzuri kwa kutoka kwa viongozi wa
mkoa huo wa kuhakikisha madawati yanapatikana.
Amesema mkoa wake ulikua na upungufu wa madawati zadi ya 66,031
yaliyokuwa yakihitajika katika shule za msingi huku Sekondari
zikihitaji madawati zaidi ya 30,000.
Amesema wabunge wa majimbo ya Dar es salaam tayari wametoa madawati
5000 kila mmoja katika yao na juhudi zinaendelea kufanywa na madiwani na
Mameya kutenga fedha kwenye bajeti za Halmashauri zao kwa ajili ya
ununuzi wa madawati.
Amewashukuru Wakuu wa wilaya kwa kuwa mstari wa mbele kuwahamasisha
wananchi na wadau mbalimbali kuchangia madawati kwa kujitolea na
kufanikisha mkoa huo kuwa umepata madawati yote yaliyobaki ifikapo
Agosti 31 mwaka huu
VYUMBA VYA MADARASA
Amesema bado mkoa unakabiliwa na uhaba wa vyumba vya madarasa na
kuongeza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe
Magufuli katika ahadi zake aliupatia mkoa huo kiasi cha shilingi bilioni
2.7 zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya madawati zihamishiwe kwenye
ujenzi wa vyumba vya madarasa na kazi ya kumalizia upatikanaji wa
madawati yaliyobaki ibaki kwa viongozi wa mkoa huo.
Amesema fedha hizo zimekwishakutengwa na kuanza kusambazwa kwenye
wilaya husika na kusisitiza kuwa ujenzi wa madarasa hayo unaendelea
lengo likiwa kujenga madarasa 123 kwa fedha zilizotolewa na Mhe.Rais
Dkt. John Magufuli.
“Kama mkoa tunamshukuru Rais alitupatia shilingi bilioni 2 na
akawabana mawaziri wake wakachanga milioni 107, tukafikisha jumla ya
shilingi bilioni 2.1 fedha hizi ilikua ziende kwenye madawati,
nikamwomba Mhe. Rais aturuhusu tuzitumie kwa ajili ya ujenzi wa madarasa
ili madawati tuendelee kupambana nayo sisi wenyewe”Amesisitiza Mhe.
Makonda.
Aidha, wadau mbalimbali kutoka ndani ya nchi wamekuwa mstari wa mbele
kuunga mkono kampeni juhudi za Serikali kwa kutoa michango mbalimbali
na kufanikisha ujenzi wa madarasa kupitia uchangiaji wa mabati mabati
10,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa pia wadau kuchangia tani zipatazo
35 za nondo.
USAFI WA MAZINGIRA.
Amesema mkoa wa Dar es salaam una changamoto ya uzalishaji wa taka
nyingi ikilinganishwa na maeneo mengine nchini kwa kuwa una idadi kubwa
ya watu takribani wakazi zaidi ya milioni 5 ambao
Amesema juhudi za kuendelea kuliweka jiji hilo katika hali ya usafi
zinaendelea kwa kuwahamasisha wananchi kujenga utamaduni wa kusafisha
mazingira yao ili kujikinga na magonjwa ya milipuko ikiwemo
kipindupindu yanayosababishwa na uchafu.
Amewataka viongozi wa mkoa huo kusimamia wajibu wa kuliweka jiji
katika hali ya usafi kwa kusimamia sheria ili jiji hilo liwe katika hali
ya usafi ikiwa ni pamoja na kuwaagiza wamiliki wa maduka yote katika
jiji hilo kuwa na vifaa vya kutupia taka nje ya maduka yao.
Amepongeza juhudi za watendaji wa mkoa huo kutenga fedha kwenye
bajeti ya 2016/2017 kwa ajili ya kununulia magari ya kubebea taka.
Ili kuhakikisha kuwa kampeni hiyo inakuwa endelevu na inafanywa kwa
kasi na nguvu kubwa ameanzisha mpango wa utoaji wa gari (pick-up) na
fedha kama motisha kwa Mwenyekiti wa mtaa atakayefanya vizuri kwenye
usafi kuanzia mwezi huu, huku wajumbe 5 wa Serikali ya mtaa na mtendaji
wa mtaa utakaofanya vizuri wakipatiwa kiasi cha shilingi milioni 5 kila
mmoja.
"Napenda kuwajulisha kuwa mwezi huu niliahidi kukabidhi gari aina ya
pick- up kwa mwenyekiti wa Serikali ya mtaa atakayefanya vizuri kwenye
usafi,kwenye mtaaa wake na tayari nimeshainunua nalenga kutoa motisha
kwa viongozi hao” Amesema.
Amesema zawadi hizo zitatolewa kwa kwa kuzingatia vigezo vya Afya
vilivyowekwa na tayari timu iliyoundwa kufuatilia suala hilo imeanza
kazi ya kupita katika maeneo mbalibali kufuatilia utekelezaji wa kampeni
hiyo kubaini mitaa na viongozi waliofanya vizuri na kusisitiza kwamba
viongozi wa mitaa watakaozembea kusimamia usafi katika maeneo yao
watatangazwa hadharani kupitia vyombo vya habari ili jamii iwajue kuwa
wanakwamisha kampeni ya usafi.
SOKO LA KARIAKOO
Mhe. Makonda amepongeza juhudi zinazofanywa na viongozi na watendaji
wa halmashauri ya Ilala na jiji kuifanya Kariakoo kuwa katika hali ya
usafi na na kuwawezesha wananchi kupita kwa urahisi tofauti na
ilivyokuwa awali.
Amesema yeye kama mkuu wa mkoa aliyekabidhiwa jukumu la kusimamia
mkoa huo atahakikisha kuwa maeneo yote ya jiji la Dar es salaam ikiwemo
Kariakoo na Ubungo yanabaki kuwa maeneo yanayowezesha wananchi kupita
kwa huru bila hofu yoyote.
“ Mimi nawapongeza Mameya wa jiji, wakuu wa wilaya, wakurugenzi na
Maafisa Biashara kwa kazi nzuri mnayoendelea kuifanya kuifanya Kariakoo
na Ubungo iweze kupitika, nawahakikishia maadam mimi ndiyo Mkuu wa Mkoa
itabaki hivyo, maeneo hayo yatabaki salama kwa watu kupita na wale
wanaofanya biashara na kulipa kodi wafanye kazi yao kwa uhuru ”
Amesisitiza.
WAMACHINGA KATIKATI YA JIJI.
Amewataka wafuate sheria zinazosimamia jiji kwa kuacha kufanya
biashara maeneo yasiyoruhusiwa na kuwa tayari kwenda kwenye maeneo
waliyopangiwa na kuongeza kuwa ataendelea kusimamia sheria, kanuni na
taratibu zinazouongoza mkoa huo kuhakikisha kuwa maeneo yaliyopangwa kwa
ajili ya wafanyabiashara hao na halmashauri husika yanatumika kama
ilivyokusudiwa ili Dar es salaam iwe mahali pazuri na salama pa kuishi.
Mhe. Makonda amekiri kuwepo kwa malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara
wenye maduka eneo la kariakoo ambao wamekua wakikwamishwa na
wafanyabiashara wadogo ambao wamekuwa wakipanga barabarani, nje ya
maduka yao bidhaa zilezile wanazouza wao katika maduka yao huku wakiwa
hawalipii kodi jambo ambalo linawasababishia hasara.
Amewaagiza wakuu wa wilaya watangaze barabara zitakazotengwa katika
kata kwa ajili ya kufungwa mwisho wa Juma (week end) ili zitumiwe na
wafanyabiashara wadogo kama alivyoagiza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania alipokuwa akiwahutubia wakazi wa jiji la Mwanza Agosti 11, 2016
na kuongeza kuwa barabara zitakazofungwa zitahusisha zile za Kata
ambazo zitakuwa zinahudumiwa na Ofisi za kata ili kuwawezesha wananchi
kufanya biashara kwa uhuru na kusimamia usafi wa mazingira katika maeneo
yao.
OMBAOMBA.
Kuhusu ombaomba amesema kuwa mkoa wake utalishughulikia kwa nama ya
kipekee kwa kuwa kumekuwa na ongezeko la ombaomba ambao wamegawanyika
katika makundi ya watu wazima na watoto ambao sasa wamekuwa kero kwa
wakihusishwa na vitendo vya ukwapuaji wa mali za watu, kuharibu magari
pindi wanapokosa fedha walizoomba kutoka kwa watumia barabara.
Amewaagiza wenyeviti wa Kamati za ulinzi na Usalama wa mkoa huo
katika kila wilaya kulifanyanyia kazi suala hilo wakishirikiana na
maafisa Maendeleo ya Jamii kuhakikisha hakuna watoto wanaozunguka
kuombaomba kwa kuwa walitakiwa kuwa shule na elimu sasa inatolewa bure.
KERO YA USAFIRI.
Amepongeza juhudi zilizofanywa na Serikali kupitia Mradi wa Mabasi ya
mwendokasi ambayo yamekuwa msaada kwa wakazi wa jiji hilo pia uwepo wa
Treni za abiria za reli ya Kati katika jiji la Dar es salaam kutokea Dar
es salaam stesheni hadi Ubungo na Pugu.
Aidha, mkoa umeiomba Wizara ya Ujenzi, Mawasliano na Uchukuzi
kuangalia uwezekano wa kuanzisha boti tatu za kisasa zitakazoanzia
safari yake Feri kwenda Mtoni Kijichi na Mbagala na wataalam wa wizara
husika wanafanya upembuzi yakinifu kuwezesha jambo hilo wakati
ukisubiriwa utekelezaji wa Awamu ya pili na tatu wa ujenzi wa mradi wa
mabasi ya mwendokasi katika jiji hilo.
Kuhusu msongamano wa malori ya mafuta yanayokuja katika Bandari ya
Dar es salaam kuchukua mafuta, mkoa huo kwa kushirikiana na Wizara ya
Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi pamoja na Wizara ya Nishati na Madini
umeweka mkakati wa kuangalia uwezekano wa kujenga bomba la mafuta
litakalotoka Kurasini hadi chalinze kupitia njia ya mradi wa Tazama
ambalo litapunguza msongamano wa malori yapatayo 1000 hadi 1500
yanayoingia na kutoka katika jiji hilo.
ULINZI NA USALAMA.
Amesema kuwa Serikali ya mkoa wa Dar es salaam itaendelea kuhakikisha
kuwa jiji la Dar es salaam linakuwa salama na kuvitaka vyombo vya
Ulinzi na Usalama hasa Jeshi la Polisi kuendelea kutekeleza sheria na
majukumu yao ipasavyo ili kudhibiti vitendo vya kiharifu na uvunjaji wa
sheria, ujambazi, umiliki silaha haramu, madawa ya kulevya, vitendo vya
udharirishaji wa binadamu .
“Kipindi cha nyuma silaha zilikua zinalia hovyo sasa nalishukuru
Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam kwa kazi nzuri,
tutaendelea kuhakikisha ulinzi na usalama unakuwepo kwa kufanya
oparesheni za wamiliki silaha kinyume cha sheria kuondoa kila aina ya
uharifu unaofanyika ndani ya majumba ya watu katika jiji hili”
Amesisitiza Mhe. Makonda.