Makonda abainisha vipaumbele vya mkoa wake


Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Paul Makonda amewataka watendaji wa mkoa huo kuhakikisha kuwa wanasimamia ubora wa madawati yanayotengenezwa na vyumba vya madarasa vinavyojengwa maeneo mbalimbali ya mkoa huo.
Aidha, amezitaka manispaa za mkoa huo kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya kujenga madarasa mapya na kuwahamasisha wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo kujitolea kufanikisha mpango huo na kutoa wito kwa madiwani kujiwekea mkakati wa kujenga walau madarasa mawili kwenye Kata zao.

RC Paul Makonda

Akifungua kikao chake cha kwanza cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Dar es salaam (RCC), Mhe Makonda amesema kuwa licha jiji hilo kukabiliwa na changamoto za kimaendeleo za muda mrefu kwenye sekta ya elimu, miundombinu ya Afya, maji na barabara mafanikio yameanza kuonekana kutokana na juhudi za pamoja za viongozi wa mkoa huo.
UPATIKANAJI WA MADAWATI
Kuhusu upatikanaji wa madawati amesema kuwa toka Mhe. Rais wa Jamhuri ya Tanzania atangaze kampeni ya upatikanaji wa madawati kwa ajili ya shule za Msingi kumekuwa na mwitikio mzuri kwa kutoka kwa viongozi wa mkoa huo wa kuhakikisha madawati yanapatikana.
Amesema mkoa wake ulikua na upungufu wa madawati zadi ya 66,031 yaliyokuwa yakihitajika katika shule za msingi huku Sekondari zikihitaji madawati zaidi ya 30,000. 
Amesema wabunge wa majimbo ya Dar es salaam tayari wametoa madawati 5000 kila mmoja katika yao na juhudi zinaendelea kufanywa na madiwani na Mameya kutenga fedha kwenye bajeti za Halmashauri zao kwa ajili ya ununuzi wa madawati.
Amewashukuru Wakuu wa wilaya kwa kuwa mstari wa mbele kuwahamasisha wananchi na wadau mbalimbali kuchangia madawati kwa kujitolea na kufanikisha mkoa huo kuwa umepata madawati yote yaliyobaki ifikapo Agosti 31 mwaka huu

VYUMBA VYA MADARASA

Amesema bado mkoa unakabiliwa na uhaba wa vyumba vya madarasa na kuongeza kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Pombe Magufuli katika ahadi zake aliupatia mkoa huo kiasi cha shilingi bilioni 2.7 zilizokuwa zimetengwa kwa ajili ya madawati zihamishiwe kwenye ujenzi wa vyumba vya madarasa na kazi ya kumalizia upatikanaji wa madawati yaliyobaki ibaki kwa viongozi wa mkoa huo.
Amesema fedha hizo zimekwishakutengwa na kuanza kusambazwa kwenye wilaya husika na kusisitiza kuwa ujenzi wa madarasa hayo unaendelea lengo likiwa kujenga madarasa 123 kwa fedha zilizotolewa na Mhe.Rais Dkt. John Magufuli.

“Kama mkoa tunamshukuru Rais alitupatia shilingi bilioni 2 na akawabana mawaziri wake wakachanga milioni 107, tukafikisha jumla ya shilingi bilioni 2.1 fedha hizi ilikua ziende kwenye madawati, nikamwomba Mhe. Rais aturuhusu tuzitumie kwa ajili ya ujenzi wa madarasa ili madawati tuendelee kupambana nayo sisi wenyewe”Amesisitiza Mhe. Makonda.

Aidha, wadau mbalimbali kutoka ndani ya nchi wamekuwa mstari wa mbele kuunga mkono kampeni juhudi za Serikali kwa kutoa michango mbalimbali na kufanikisha ujenzi wa madarasa kupitia uchangiaji wa mabati mabati 10,000 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa pia wadau kuchangia tani zipatazo 35 za nondo.


USAFI WA MAZINGIRA.
Amesema mkoa wa Dar es salaam una changamoto ya uzalishaji wa taka nyingi ikilinganishwa na maeneo mengine nchini kwa kuwa una idadi kubwa ya watu takribani wakazi zaidi ya milioni 5 ambao 

Amesema juhudi za kuendelea kuliweka jiji hilo katika hali ya usafi zinaendelea kwa kuwahamasisha wananchi kujenga utamaduni wa kusafisha mazingira yao ili kujikinga na magonjwa ya milipuko ikiwemo kipindupindu yanayosababishwa na uchafu.

Amewataka viongozi wa mkoa huo kusimamia wajibu wa kuliweka jiji katika hali ya usafi kwa kusimamia sheria ili jiji hilo liwe katika hali ya usafi ikiwa ni pamoja na kuwaagiza wamiliki wa maduka yote katika jiji hilo kuwa na vifaa vya kutupia taka nje ya maduka yao.

Amepongeza juhudi za watendaji wa mkoa huo kutenga fedha kwenye bajeti ya 2016/2017 kwa ajili ya kununulia magari ya kubebea taka.


Ili kuhakikisha kuwa kampeni hiyo inakuwa endelevu na inafanywa kwa kasi na nguvu kubwa ameanzisha mpango wa utoaji wa gari (pick-up) na fedha kama motisha kwa Mwenyekiti wa mtaa atakayefanya vizuri kwenye usafi kuanzia mwezi huu, huku wajumbe 5 wa Serikali ya mtaa na mtendaji wa mtaa utakaofanya vizuri wakipatiwa kiasi cha shilingi milioni 5 kila mmoja.

"Napenda kuwajulisha kuwa mwezi huu niliahidi kukabidhi gari aina ya pick- up kwa mwenyekiti wa Serikali ya mtaa atakayefanya vizuri kwenye usafi,kwenye mtaaa wake na tayari nimeshainunua nalenga kutoa motisha kwa viongozi hao” Amesema.
Amesema zawadi hizo zitatolewa kwa kwa kuzingatia vigezo vya Afya vilivyowekwa na tayari timu iliyoundwa kufuatilia suala hilo imeanza kazi ya kupita katika maeneo mbalibali kufuatilia utekelezaji wa kampeni hiyo kubaini mitaa na viongozi waliofanya vizuri na kusisitiza kwamba viongozi wa mitaa watakaozembea kusimamia usafi katika maeneo yao watatangazwa hadharani kupitia vyombo vya habari ili jamii iwajue kuwa wanakwamisha kampeni ya usafi.

SOKO LA KARIAKOO
Mhe. Makonda amepongeza juhudi zinazofanywa na viongozi na watendaji wa halmashauri ya Ilala na jiji kuifanya Kariakoo kuwa katika hali ya usafi na na kuwawezesha wananchi kupita kwa urahisi tofauti na ilivyokuwa awali.

Amesema yeye kama mkuu wa mkoa aliyekabidhiwa jukumu la kusimamia mkoa huo atahakikisha kuwa maeneo yote ya jiji la Dar es salaam ikiwemo Kariakoo na Ubungo yanabaki kuwa maeneo yanayowezesha wananchi kupita kwa huru bila hofu yoyote.
“ Mimi nawapongeza Mameya wa jiji, wakuu wa wilaya, wakurugenzi na Maafisa Biashara kwa kazi nzuri mnayoendelea kuifanya kuifanya Kariakoo na Ubungo iweze kupitika, nawahakikishia maadam mimi ndiyo Mkuu wa Mkoa itabaki hivyo, maeneo hayo yatabaki salama kwa watu kupita na wale wanaofanya biashara na kulipa kodi wafanye kazi yao kwa uhuru ” Amesisitiza.

WAMACHINGA KATIKATI YA JIJI.
Amewataka wafuate sheria zinazosimamia jiji kwa kuacha kufanya biashara maeneo yasiyoruhusiwa na kuwa tayari kwenda kwenye maeneo waliyopangiwa na kuongeza kuwa ataendelea kusimamia sheria, kanuni na taratibu zinazouongoza mkoa huo kuhakikisha kuwa maeneo yaliyopangwa kwa ajili ya wafanyabiashara hao na halmashauri husika yanatumika kama ilivyokusudiwa ili Dar es salaam iwe mahali pazuri na salama pa kuishi.

Mhe. Makonda amekiri kuwepo kwa malalamiko kutoka kwa wafanyabiashara wenye maduka eneo la kariakoo ambao wamekua wakikwamishwa na wafanyabiashara wadogo ambao wamekuwa wakipanga barabarani, nje ya maduka yao bidhaa zilezile wanazouza wao katika maduka yao huku wakiwa hawalipii kodi jambo ambalo linawasababishia hasara.

Amewaagiza wakuu wa wilaya watangaze barabara zitakazotengwa katika kata kwa ajili ya kufungwa mwisho wa Juma (week end) ili zitumiwe na wafanyabiashara wadogo kama alivyoagiza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alipokuwa akiwahutubia wakazi wa jiji la Mwanza Agosti 11, 2016 na kuongeza kuwa barabara zitakazofungwa zitahusisha zile za Kata ambazo zitakuwa zinahudumiwa na Ofisi za kata ili kuwawezesha wananchi kufanya biashara kwa uhuru na kusimamia usafi wa mazingira katika maeneo yao.

OMBAOMBA.
Kuhusu ombaomba amesema kuwa mkoa wake utalishughulikia kwa nama ya kipekee kwa kuwa kumekuwa na ongezeko la ombaomba ambao wamegawanyika katika makundi ya watu wazima na watoto ambao sasa wamekuwa kero kwa wakihusishwa na vitendo vya ukwapuaji wa mali za watu, kuharibu magari pindi wanapokosa fedha walizoomba kutoka kwa watumia barabara. 
Amewaagiza wenyeviti wa Kamati za ulinzi na Usalama wa mkoa huo katika kila wilaya kulifanyanyia kazi suala hilo wakishirikiana na maafisa Maendeleo ya Jamii kuhakikisha hakuna watoto wanaozunguka kuombaomba kwa kuwa walitakiwa kuwa shule na elimu sasa inatolewa bure. 

KERO YA USAFIRI.
Amepongeza juhudi zilizofanywa na Serikali kupitia Mradi wa Mabasi ya mwendokasi ambayo yamekuwa msaada kwa wakazi wa jiji hilo pia uwepo wa Treni za abiria za reli ya Kati katika jiji la Dar es salaam kutokea Dar es salaam stesheni hadi Ubungo na Pugu.
Aidha, mkoa umeiomba Wizara ya Ujenzi, Mawasliano na Uchukuzi kuangalia uwezekano wa kuanzisha boti tatu za kisasa zitakazoanzia safari yake Feri kwenda Mtoni Kijichi na Mbagala na wataalam wa wizara husika wanafanya upembuzi yakinifu kuwezesha jambo hilo wakati ukisubiriwa utekelezaji wa Awamu ya pili na tatu wa ujenzi wa mradi wa mabasi ya mwendokasi katika jiji hilo.
Kuhusu msongamano wa malori ya mafuta yanayokuja katika Bandari ya Dar es salaam kuchukua mafuta, mkoa huo kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi pamoja na Wizara ya Nishati na Madini umeweka mkakati wa kuangalia uwezekano wa kujenga bomba la mafuta litakalotoka Kurasini hadi chalinze kupitia njia ya mradi wa Tazama ambalo litapunguza msongamano wa malori yapatayo 1000 hadi 1500 yanayoingia na kutoka katika jiji hilo.

ULINZI NA USALAMA.

Amesema kuwa Serikali ya mkoa wa Dar es salaam itaendelea kuhakikisha kuwa jiji la Dar es salaam linakuwa salama na kuvitaka vyombo vya Ulinzi na Usalama hasa Jeshi la Polisi kuendelea kutekeleza sheria na majukumu yao ipasavyo ili kudhibiti vitendo vya kiharifu na uvunjaji wa sheria, ujambazi, umiliki silaha haramu, madawa ya kulevya, vitendo vya udharirishaji wa binadamu . 
“Kipindi cha nyuma silaha zilikua zinalia hovyo sasa nalishukuru Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es salaam kwa kazi nzuri, tutaendelea kuhakikisha ulinzi na usalama unakuwepo kwa kufanya oparesheni za wamiliki silaha kinyume cha sheria kuondoa kila aina ya uharifu unaofanyika ndani ya majumba ya watu katika jiji hili” Amesisitiza Mhe. Makonda.
 

Post a Comment

Previous Post Next Post