SHINYANGA YAONGOZA NDOA ZA UTOTONI


Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Watoto wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Magreth Mussai 

NA VERONICA ROMWALD, DAR ES SALAAM

MKOA wa Shinyanga unaongoza kwa kuwa na kiwango kikubwa cha ndoa za utotoni kwa asilimia 59.

Vilevile, asilimia 42 ya wasichana   barani Afrika huolewa wakiwa na umri wa chini ya miaka 18.

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya Watu (UNFPA) linakadiria kuwa miaka 10 ijayo wasichana wapatao milioni moja wanatarajiwa kuolewa katika umri huo.

Kaimu Mkurugenzi wa Maendeleo ya Watoto wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Magreth Mussai (pichani juu) alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Mtoto wa Kike.

Alitaja mikoa mingine yenye ndoa za utotoni na asilimia zake kuwa ni Tabora asilimia 58, Mara 55, Dodoma 51, Lindi 48, Mbeya 45, Morogoro 42, Singida 42, Rukwa 40 na Ruvuma 39.

Nyingine ni Mwanza 37, Kagera 36, Mtwara 35, Manyara 34, Pwani 33, Tanga 29, Arusha 27, Kilimanjaro 27, Kigoma 29, Dar es Salaam 19 na Iringa asilimia nane.

“Kwa kuwa Shinyanga inaongoza kwa kuwa na kiwango kikubwa cha ndoa za utotoni, serikali na wadau wameona vema maadhimisho hayo yafanyike mkoani humo Oktoba 11, mwaka huu kuelimisha jamii.

“Kiwango cha ndoa za utotoni nchini kipo kwa kiwango kikubwa na wasichana wengi wanaoolewa wanatoka kwenye familia maskini na wale wanaoishi   vijijini.

“Takwimu zinaonyesha asilimia 61 ya wanawake wenye umri kati ya miaka 20 hadi 24 ambao hawakusoma na asilimia 39 ya wanawake wenye umri huo wenye elimu ya msingi ndiyo walioolewa wakiwa chini ya umri wa miaka 18,” alisema.

Alisema hali hiyo inafanya ndoa za utotoni kuwa ni sehemu ya unyanyasaji wa watoto wa kike.

Post a Comment

Previous Post Next Post