Mbunge wa Singida Mashariki Tundu Lisu akipelekwa mahabusu kwa jili ya kusubiri kupandishwa kizimbani
Tundulisu akishuka kwenye gari akiwa amebeba suti yake
Tundu Lisu akielekea Rumande kwa ajili ya kusubiri kupandishwa kizimbani
Na Karama Kenyunko
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeitupilia
mbali hati ya kiapo ya mkuu wa upelelezi Ilala, Mrakibu Msaidizi wa Polisi,
Denis Mujumba na kumuachia Tundu lissu kwa dhamana.
Lissu yuko nje kwa dhamana ya
shilingi milioni ishirini na mdhamini mmoja.
Hatua hiyo imekuja baada ya upande wa
mashtaka kumsomea Lissu ambaye ni Mbunge na mnadhimu mkuu wa kambi ya upinzani
mashtaka yake na kuwasilisha hati ya kiapo kupinga mbunge huyo kupewa dhamana.
Hakimu Mkazi Mkuu wa mahakama hiyo
alisema kuwa kiapo kilichowasilishwa mahakamai hapo na upande wa mashtaka kina
mapungufu makubwa sana.
Amesema kuwa kukosekana kwa namba ya
kesi na mahali ambapo inaonyesha muapaji wa kiapo hicho aliapa ni mapungufu
makubwa.
Ameongeza kuwa mshtakiwa Lissu
anahaki ya kupata dhamana kwa kuwa shtaka analikabiliwa nalo linadhaminika
licha ya kuwa na kesi tatu tofauti mahakamani hapo kama ambapo kiapo
kilivyosema.
Amesema kuwa, licha ya kuwa Lissu
kweli anamashtaka mahakamani hapo lakini hakuna shtaka hata moja ambalo amekutwa
na hatia na alilokutwa nalo na hatia Kabla ya kiapo hicho jopo la mawakili wanne
likiongozwa na wakili Mwandamizi wa Serikali Mutalemwa Kishenyi aliyekuwa
akisaidiana na Wakili Easter Martin, Jackline Nyantori na Clementina Masawe
walimsomea mshtakiwa mashtaka yake manne yanayomkabili ya kutoa lugha ya
uchochezi.
Lissu ambaye amefikishwa katika
viwanja vya mahakama hiyo leo majira ya saa 11.42 asubuhi akiwa ndani ya land
lover ya polisi pamoja na msanii maarufu wa uigizaji nchini Wema Sepetu na
watuhumiwa wengine alikamatwa juzi mara baada ya kutoka kwenye viwanja vya
Bunge mjini Dodoma. Saa 12:24 mchana, Lissu alipandishwa kizimbani Mbele ya
Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi, Wakili wa Serikali Mwandamizi, Mutalemwa
Kishenyi alidai kuwa mshtakiwa huyo anakabiliwa na makosa manne ya kutoa lugha
ya uchochezi.
Katika kesi hiyo namba 48 ya mwaka
2017, Lissu anatetewa na mawakili watano, Peter Kibatala, Omary Msemo, John
Mallya na Fredrick Kihwelo.Jeremiah Ntobesya.
Wakili Kishenyi alidai kuwa Januari
11, mwaka huu maeneo ya Kibunju Maungoni maeneo ya Magharibi B wilaya ya Mjini
Magharibi mkoa wa Zanzibar Lissu alitoa matamko mbalimbali ya uchochezi
Moja kati ya mashtaka hayo ni kwamba
mshtakiwa Lissu akiwa kama Mtanzania kutoka Bara, kabla ya uchaguzi mdogo wa
ubunge jimbo la Dimani, ambapo akiwa kwenye Kampeni alisema kuwa “…Tangu mwaka
1964 Tanganyika ndiyo inayoamua nani atawale Zanzibar…”. Kishenyi alidai kuwa
maneno hayo yangesababisha uvunjifu wa amani.
Mshtakiwa Lissu alipoulizwa kama ni
kweli ametenda makosa hayo, alikubaliana na makosa yote na kudai kuwa ni kweli
alisema hayo maneno lakini kusema ukweli sio kosa la jinai, hivyo jibu lake ni
hapana.
Matamko mengine anayodaiwa kutamka
Lissu ni kuwa, “…Tangu mwaka 1964
Zanzibar inakaliwa Kijeshi na Tanganyika, nane anaye bisha…Tangu mwaka 1995
ikifika uchaguzi askari wa Tanganyika wanahamia Zanzibar ili kuja kuhakikisha
vibaraka wao wa Zanzibar hawaondolewi madarakani na wananchi wa Zanzibar
mnapigwa,
Mnateswa, mnauawa kwa sababu ya
ukoloni wa Tanganyika kwa Zanzibar….,Marehemu Karume alipoanza kushtakiwa mwaka
71, 72 akauawa…itakapofika tarehe 15 mwezi wa kwanza muadhimishe miaka 53 ya
kukaliwa kijeshi na Tanganyika…,”.
Aidha inadaiwa kuwa, siku na mahali
hapo Lissu akiwa kwenye kampeni za uchaguzi mdogo jimbo la Dimani alisema kuwa
“…Jumbe aliondolewa Dodoma, na Ally Hassan Mwinyi alipewa urais wa Zanzibar
Dodoma, na aliyempa ni Nyerere na si Wazanzibar…, marais wa Zanzibar wote ni
made in Tanganyika…, wametengenezwa Tanganyika, wako madarakani kwa sababu ya
Tanganyika,”.
Katika shtaka la mwisho la kutoa
lugha ya uchochezi kwa kutamka kuwa
“…Zanzibar wanatawaliwa na Tanganyika
kwa kivuli cha Tanzania, Tanzania ni Tanganyika…, Tanzania ni kivuli tu cha
kuikalia Zanzibar, cha kuigeuza Zanzibar koloni, na makoloni uwa yananyonywa,
Yananyonywa kisiasa, kiuchumi na
yanakandamizwa kijeshi…Metawaliwa na Tanganyika kisiasa miaka yote hii…,
Mohamed Shein hana lolote ni kibaraka tu siku watawala wakisema hatufai
ataondolewa tu kama alivyo ondolewa Aboud Jumbe…,”.
Kishenyi alidai kuwa maneno hayo ya
Lissu yangesababisha uvunjifu wa amani.
Baada ya kusoma mashtaka hayo upande
wa serikali ulidai kuwa upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika na kuomba kesi
hiyo iahirishwe.
Aidha aliomba mahakama kuzuia dhamana
kwa mshtakiwa, maombi ambayo yanaungwa mkono na kiapo kutoka kwa Mkuu wa
Upelelezi wa Makosa ya Jinai Ilala, ASP
Mujumba.
Kiapo hicho kimewasilishwa kikiwa na
hoja kadhaa ya kutaka Lissu akose dhamana ikiwemo ya kukabiliwa na kesi tatu
katika mahakama hiyo ikiwemo namba 279/2016, 218/2016 na 233/2016.
Hata hivyo Hakimu Shahidi baada ya
kupitia hoja zote zilizotolewa na upande wa utetezi na ule wa serikali alifikia
uamuzi kuwa,mshtakiwa anahaki ya kupata dhamana kwa kuwa shtaka linalomkabili
inadhaminika na kwamba hati hiyo ya kiapo inamapungufu sana.
Tundulisu akishuka kwenye gari akiwa amebeba suti yake
Tundu Lisu akielekea Rumande kwa ajili ya kusubiri kupandishwa kizimbani