TEMBO ZAIDI YA 20 WAHARIBU EKARI 50 ZA MAZAO

Tembo zaidi ya 20 wamevamia vijiji vya Wenje mpakani mwa Tanzania na Msumbiji wakitokea nchini Msumbiji ambapo tembo wawili wameuawa na wananchi na kuondolewa meno mawili na kugawana nyama yao huku tembo wengine zaidi ya 30 wakivamia kijiji cha jakika wakitokea Pori la Akiba la Selou na kuharibu zaidi ya ekari 50 za mazao mbalimbali.

Hayo yameelezwa na Kaimu Afisa wanyamapori wa wilaya ya Tunduru Bw.Limbega Hassan aliyeongoza kikosi cha askari  wanyamapori waliokuwa wakiangalia usalama wa tembo na wananchi ambapo wananchi wamemng’oa meno mawili tembo mmoja na kuondoka nayo  huku meno mawili ya tembo mwingine yakisalimishwa kituo cha polisi cha Tunduru.

Kaimu Afisa wanyamapori  huyo wa wilaya ya Tunduru anasema kuwa wamewakamata watu watano wanaodaiwa kuhusika na kuwaua tembo wawili na kutoweka na meno huku wekiwatafuta wengine wawili  wawachukulie hatua na pia mikakati ikiwekwa  kuwadhibiti tembo katika vijiji vitano vinavyosumbuliwa na tembo.

Hata hivyo pamoja na makundi makubwa ya  tembo kuingia kwenye vijiji na kuleta taharuki  mkuu wa wilaya Tunduru Bw. Juma Homera amesema kuwa hali ya usalama  iko shwari  askari wanyamapori wamefanikiwa kuwadhibiti tembo hao na hakuna  mwananchi aliyedhurika.

CHANZO: ITV TANZANIA

Post a Comment

Previous Post Next Post