NA VERONICA ROMWALD – DAR ES SALAAM
BIDHAA pekee ambayo miaka ya nyuma ilikuwa ikitumika
kumuhifadhi mtoto pindi anapojisaidia haja ndogo au kubwa ilikuwa nepi na chupi
maalumu maarufu chupi ya mkojo.
Lakini kadri siku zinavyosonga mbele kumekuwa na mabadiliko
makubwa ya kitekonolojia leo hii kuna bidhaa mpya inayotumika ambayo imejizolea
umaarufu mkubwa (pampasi).
Kwa kawaida pampers hutofautiana bei kulingana na ukubwa,
aina na kiwanda ilikotengenezwa lakini huwa ni kati ya Sh 10,000 na zaidi.
Frolence Mussa (si jina lake halisi), mkazi wa Mbezi ni mama
wa mtoto mmoja mwenye umri wa mwaka mmoja.
Anasema huwa anatumia bidhaa zote mbili (nepi na pampasi)
kumsitiri mtoto wake lakini huwa inategemea na sehemu alipo.
“Kwa mfano nikiwa nyumbani huwa namvalisha nepi na mara
nyingi huwa ni kipindi cha usiku tunapokwenda kulala lakini tunapotoka kwenda
safari au kanisani huwa namvalisha pampasi,” anasema.
..
Florence anasema mchana huwa hamvalishi nepi wala pampers
badala yake humvalisha kamputa pekee na kumbadilisha kila anapojisaidia.
“Sipendi kumvalisha nepi wala pampers mchana maana wakati
mwingine huwa zinamchubua, hasa pampasi,” anasema.
Anasema hata hivyo wakiwa wamekwenda safari humvalisha pampasi
na ikiwa anakuwa hajajisaidia haja kubwa ukaa nayo kwa saa sita.
“Huwa namuacha anakaa nayo hata saa sita, si anakuwa
amejisaidia haja ndogo tu lakini inapotokea amejisaidia haja kubwa inabidi
nimbadilishe.
“Napenda kutumia pampasi zaidi tukiwa safari maana anakaa
nayo muda mrefu kunakuwa hakuna ule usumbufu wa kumbadilisha kila mara, si kama
nepi yenyewe unalazimika kumbadilisha mara kwa mara,” anasema.
Shija Mabula ambaye ni baba wa mtoto mmoja anasema huwa
anapenda zaidi mtoto wake avae pampasi kuliko nepi.
“Pampasi anakaa nayo muda mrefu hata zaidi ya saa mbili ikiwa
hajajisaidia haja ndogo mara nyingi au kubwa. Huwa tunamvalisha zaidi usiku na
tukiwa safari,” anasema.
Je kuna
athari gani
Shija na Florence wote hawajui iwapo hatua yao hiyo inaweza
kuwasababishia matatizo watoto wao wapendwa katika maisha yao siku zijazo.
MTANZANIA limefanya mahojiano na Daktari Bingwa wa Magonjwa
ya Watoto katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Gudila Valentine na hapa
anaeleza athari anazoweza kuzipata mtoto kutokana na hatua hiyo.
“Ni hatari kumuacha mtoto muda mrefu akiwa amevaa pampers
moja kwani inaweza kumsababishia kupata magonjwa ya UTI na baadae anaweza
kupata ugonjwa sugu la figo,” anasema.
Inakuwaje
Dk. Gudila ambaye kwa sasa anasomea ubingwa katika magonjwa
ya figo kwenye Chuo Kikuu Kishirikishi cha Sayansi ya Tiba (Muhas) anafafanua,
“Mtoto akikaa na pampasi au nepi muda mrefu ni hatari kwani
husababisha mtoto kupata maambukizi, iwapo anakuwa amejisaidia muda mrefu na
kukaa na pampasi au nepi yake, kile kinyesi kinakuwa kama kinarudi, kuelekea
kwenye njia ya mkojo.
“Bakteria anayesababisha UTI anaishi kwenye sehemu ya haja
kubwa, kwa hiyo lazima mtoto naye asafishwe mara kwa mara kama ilivyo kwa watu
wazima ili kumkinga dhidi ya maambukizi ya ugonjwa huu,” anasema.
Anasisitiza “Lazima usafi uwe kitu cha kwanza. Kwa kuwa
bakteria yupo kwenye kinyesi, kinapokaa pale kwa muda mrefu hasa akiwa ni mtoto
wa kike kinapata nafasi ya kupanda na
kurudi kwenye njia ya mkojo kwa sababu zile njia zimekaa karibu karibu, hivyo
inakuwa rahisi kwa yeye kupata UTI.
Anasema ndiyo maana huwa inashauriwa wasafishwe na
kubadilishwa nepi au pampasi mara kwa mara kwamba usafi ni suala la msingi na wale
watoto wakubwa wasafishwe kutoka mbele kwenda nyuma.
Sababu
nyinginezo
Anasema wapo watu ambao hudhani kuwa watoto huwa haugui
magonjwa ya figo jambo ambalo si kweli.
“Watoto nao wanaugua magonjwa ya figo kama ilivyo kwa watu
wazima, mara nyingi visababishi kwa watoto ni pamoja na hayo magonjwa ya
maambukizi kwa mfano ya kuziba kwa njia ya mkojo (UTI) ya kujirudia rudia na kuharisha
ambako hutokana na homa ya virusi,” anasema.
Daktari huyo anasema sababu nyingine ni kutapika ambapo husababisha mwili wa mtoto
kupoteza maji mengi na kupelekea magonjwa ya figo baadae.
“Kuna magonjwa mengine kama maambukizi ya Virusi Vya Ukimwi
(VVU), homa ya ini na malaria sugu, yote haya yanaweza kusababisha mtoto kupata
magonjwa ya figo,” anasema.
Dk. Gudila anasema mtoto mwenye lishe duni naye huwa kwenye
hatari ya kupata tatizo la figo.
“Mtoto akiwa na lishe duni hupata utapiamlo ambao huchochea
baadae kupata magonjwa ya figo, matumizi mabaya ya dawa za kutuliza maumivu jamii
ya diclofenac na dawa za kienyeji ambazo
huwa zinatokewa bila kiwango maalumu, zote hizi zinaweza kusababisha mtoto
kupata magonjwa ya figo,” anasema.
Anasema kuna baadhi ya magonjwa ya kuzaliwa nayo kama kuziba
njia ya mkojo, na mengine mtoto hurithi toka kwa wazazi wake ambayo yanaweza
kumsababishia magonjwa ya figo maishani mwake.
Utajuaje
njia ya mkojo imeziba.
Dk. Gudila anasema kitu ambacho mzazi ataweza kukiona mapema
ni kwamba atakuta mtoto hapati mkojo vizuri mara tu baada ya kuzaliwa, au
akikojoa unakuwa na damu au mtoto.
“Mzazi anapoona mkojo wa mtoto wake unatoka kwa kusita sita
au kiwango cha mkojo wa mwanawe kinapungua amuwahishe mapema ili afanyiwe
uchunguzi,” anasema.
Anaongeza “Inapokuwa hivyo ajue tayari kuna shida, au mkojo
ukitoka vitone vitone ni tatizo, kawaida mtoto akikojoa mkojo ule unatakiwa
uruke mbali lakini si kutoka kidogo.
Anasema mtoto anapokuwa amezaliwa ndani ya saa 24 mama
anatakiwa awe ameona mwanawe ameanza kujisaidia haja ndogo.
“Sasa unakuta mtoto kakaa hata siku tatu hajakojoa mama
hashtuki kama ni tatizo anaendelea kukaa naye nyumbani baadae sasa ndipo
anaanza kuvimba mwili,” anasema.
Magonjwa
mengineyo
Daktari huyo anasema magonjwa ya saratani nayo huweza
kusababisha mtoto kupata magonjwa ya figo.
“Kwa mfano saratani ya mfuko wa mkojo ambayo tunaiita kitaalamu
‘blader cancer”, anaweza pia kuugua magonjwa ya ndani ya figo ambayo mara
nyingi shida huwa inatokea pale kwenye chujio la figo,” anasema.
Jinsi ya
kumkinga
Anasema jambo la msingi ni kufuata zile kanuni za afya.
“Tunashauri mtoto anyonyeshwe miezi sita yote ya kwanza baada
ya kuzaliwa bila kupewa chakula kingine, inamsaidia kupata lishe bora na ni
njia nzuri ya kumkinga na maradhi mbalimbali ikiwamo kuharisha, utapiamlo,
maambukizi na mengineyo,” anasema.
Anasema mama ahudhurie kliniki mara kwa mara kwani huko
hupewa elimu ya jinsi ya kumkinga mwanawe na magonjwa mbalimbali ukiwamo huo wa
figo.
“Kliniki wanapewa chanjo pia ambazo huwakinga na magonjwa
mengi, mtoto akiugua mpeleke hospitalini atibiwe na si kununua dawa kiholela,”
anasema.
Ushuhuda
Asha Juma (si jina lake halisi) anasema kuna changamoto
nyingi katika kulea mtoto mwenye tatizo la figo.
“Mwanangu ana miaka miwili sasa, alianza kuvimba macho,
nilipomlaza kifudi fudi akiamka macho yake yalikuwa yamevimba,” anasema.
Anasema alimpeleka katika kituo cha afya ambapo hawakugundua
tatizo lake wakarudi nyumbani.
“Kadri siku zilivyoenda mbele ndivyo hali ilivyozidi kuwa
mbaya, ukuaji wake ulikuwa si mzuri, nywele zake hazikuota vizuri, miguu na tumbo
lake likaanza kuvimba,” anasimulia.
Asha anasema aliamua kumpeleka Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya
Mwananyamala ambapo aligundulika kuwa na ugonjwa wa figo.
“Waligundua figo yake ina matundu ambayo yanaruhusu maji
kuingia mwilini ndiyo maana anavimba miguu na tumbo,” anasema.
Anasema alipewa rufaa ya kwenda Hospitali ya Taifa Muhimbili
ambako anatibiwa hadi leo.
“Pengine ingegundulika mapema asingekuwa na hali mbaya maana
alikuwa akipata malaria mara kwa mara, homa, mafua, na UTI,” anasema kwa
huzuni.
Anaongeza “Madaktari walinieleza huenda amerithi kwa sababu
kwenye familia ya mume wangu wapo ambao wanaugua ugonjwa huu.
Anasema changamoto kubwa anayoipata ni kukaa muda mwingi
akimtunza mtoto wake huyo na kushindwa kufanya shughuli zake za kiuchumi.
“Sitakiwi kumpa maji mengi, tatizo kwa kuwa ameanza kutembea
wakati mwingine akiyakuta anakunywa mengi inakuwa tatizo,” anasema.
Mnh
inapokea 30 hadi 40 kila mwezi
Daktari Bingwa wa Magonjwa ya watoto na figo Muhimbili,
Jacqueline Shoo (pichani) anasema wanapokea watoto 30 hadi 40 kila mwezi kwenye kliniki
yao wakisumbuliwa na magonjwa hayo.
“Asilimia kubwa ya watoto tunaowaona wanaugua magonjwa sugu
ya figo sawa na asilimia 60, kuliko magonjwa ya figo ya mshtuko,” anasema.
Chanzo
Anasema sababu kubwa waliyogundua kuwa chanzo cha watoto wanapokea
kupata magonjwa hayo ni maambukizi, magonjwa ya kuharisha, UTI na malaria sugu.
“Magonjwa ya kuziba kwa njia ya mkojo, matumizi ya madawa
lakini saratani zipo kwa kiasi kidogo mno,” anasema.