PSPTB IMESEMA WOGA WA WANAFUNZI UMEPUNGUZA UDAHILI KATIKA MITIHANI YA BODI HIYO

Na Humphrey Shao Globu ya Jamii
BODI ya Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB) imesema kuwa udahili wa wanafunzi wanaofanya mitihani ya bodi hiyo umepungua kutokana na woga wa wanafunzi hao na kwamba somo la hesabu limekuwa tatizo kubwa.
Akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dar es Salaam, Kaimu Mkurugenzi wa bodi hiyo, Godfred Mbanyi alisema kuwa lengo la bodi hiyo ni kudahili wanafunzi waliochukua kozi ya ununuzi na ugavi 2,000 lakini tangu mwaka 2016, udahili umekuwa ukishuka.
Amesema kuwa katika mtihani uliofanyika mwaka 2016, walifanya udahili kwa wanafunzi 1,519, waliofanya mtihani ni 1,442, waliofaulu 660 na wanafunzi 745 wanarudia mitihani huku wanafunzi 37 ambayo ni sawa na asilimia 2.6 walifeli.
Alifafanua kuwa udahili wa mwaka huu ulifanyika kwa wanafunzi 1,964 na kwamba wanafunzi 1,578 ndio waliofanya mitihani na 653 wamefaulu mitihani hiyo.
‘’Kutokana na masomo ya ugavi kuhusisha somo la hesabu, kumekuwa na matokeo hafifu kwa wanafunzi wetu wanaofanya mitihani hii ya bodi na tatizo hili limetokea hata mwaka jana. Sababu za watu kufeli masomo haya ni kwa sababu hawapendi hesabu,’’ alisema Mbanyi.
Aliongeza kuwa ‘’Wanafunzi wengi wanaofanya mitihani wanakuwa na background mbaya katika somo la hesabu hivyo tunaendelea kuweka msisitizo kwenye vituo vya maandalizi. Lakini woga wa wwanafunzi unachangiwa na kuwa na mtaala mpya wa mitihani ulioanza Novemba 2016  ambao haukuwepo na unautaratibu mpya wa ufaulu hivyo wanafunzi waliogopa.’’
Pia alisema kuwa somo la  viashiria vya hatari  katika ununuzi na ugavi  ambalo linalenga kutambua na kuainisha viashiria ili kuviepuka wakati wa mchakato wa ununuzi na kwamba masomo ya kujifunzia (case studies) watahiniwa walifeli.
‘’Udahili umepungua lakini tumeweka mikakati ya kutembelea vyuo vyote vikuu na vinavyotoa masomo ya ugavi na ununuzi kwa ngazi ya shahada na stashahada kuwahamasisha kufanya mitihani ya bodi ili watambuliwe na waongezeka,’’ alisisitiza Mbanyi.
Alieleza kuwa bodi hiyo imewataka wanafunzi wanaotaka kufanya mitihani hiyo kupitia katika vituo vya kutolea mafunzo vilivyosajiliw na bodi kwa kuwa sababu za wanafunzi kufeli mitihani hiyo inachangiwa na kutojiandaa vizuri.
Kwa mujibu wa Mbanyi, PSPTB imeweka mkakati wa kuwa na vitabu maalumu ya kufundishia vya aina moja vitakavyotumika katika vyuo vyote nchini na mitihani ijayo itakayoanza wawe wameanzisha vitabu hivyo ili kuondoa mkanganyiko katika kufundishia.
Mbanyi alisema watahakikisha kuwa wataalamu wanaozalishwa wanakuwa na mtazamo wa kufikia uchumi wa viwanda kwa kusoma masomo ya sayansi na hesabu na kwamba utaalamu wa ununuzi na ugavi utaleta matokeo chanya kufikia uchumi huo.
‘’Vyuo vinavyoongoza kwa kuleta wanafunzi wengi ni Chuo cha Ushirika Moshi (MoCU),  Taasisi ya Uhasibu Tanzania (TIA), Chuo Kikuu cha Mzumbe, Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUT), Chuo cha Biashara (CBE) na vyuo vinavyochangia ni Chuo cha Jordan Morogoro na Chuo cha Usafirishaji (NIT),’’ alifafanua.
Alisema kuwa vyuo vilivyopo Zanzibar pia vimekuwa vilileta watahiniwa kwa ajili ya kufanya mitihani hiyo ya bodi ili kuingizwa katika orodha ya wataalamu wa masuala ya ununuzi na ugavi.
Kaimu Mkurugenzi wa bodi  ya  Wataalamu wa Ununuzi na Ugavi (PSPTB), Godfred Mbanyi  akizungumza na Waandishi wa Habari wakati wanatangaza matokeo ya wanafunzi waliofanya mitihani ya bodi hiyo mwezi wa Novemba mwaka jana.
Waandishi wa Habari wakifatilia kwa makini Mkutano huo ambao ulikuwa wa kutangaza matokeo na mwenendo wa matokeo ya Mitihani kwa wanafunzi wanaokuja kujiandikisha.

Post a Comment

Previous Post Next Post