CHEMBA WAKOSA HUDUMA ZA AFYA KWA MIAKA MINNE


WANANCHI wa Kijiji cha Magasa, Kata ya Mrijo wilayani Chemba, wamekosa huduma za afya kwa muda mrefu, licha ya jengo la zahanati yao kukamilika kwa zaidi ya miaka minne sasa.
Wakizungumza na Ripota wa Jijiletu  mwishoni mwa wiki, wananchi hao walisema wanalazimika kutembea zaidi ya kilomita saba hadi vijiji vya Soya na Mrijo kufuata huduma za afya, jambo ambalo limekuwa kero kubwa kwao.
Jengo hilo ambalo limejengwa kwa nguvu za wananchi na baadae Serikali kumalizia, linadaiwa kukaa kama pambo kijijini hapo bila huduma zozote, licha ya ujenzi wake kukamilika tangu 2014.
“Jengo letu tangu limekamilika linazaidi ya miaka minne, pia tumeletewa daktari hapa alikuja kuripoti, tuliambiwa baada ya mwezi mmoja atakuja kuanza kazi, tumesubiria hadi leo hatujamwona,” alisema Ramadhan Rajabu.
Mwananchi mwingine Hamisi Kijaji alisema kinachowaumiza zaidi ni pale wajawazito wanavyopata shida, kwani wanatumia usafiri wa baiskeli na mikokoteni na wakati mwingine wanapoteza maisha njiani kutokana na ubovu wa barabara.
Kaimu Ofisa Mtendaji wa Kijiji hicho, Mussa Ninga, alikiri kukosekana kwa huduma hiyo na kueleza watumishi wawili wameripoti kijijini hapo, lakini waliondoka katika mazingira ya kutatanisha.
Ninga alimtaja daktari mmoja kwamba aliripoti kijijini hapo Novemba 28, mwaka jana akitokea Kituo cha Afya Makorongo, lakini aliondoka bila taarifa ambapo hadi sasa haijulikani alipo.
“Awali tuliletewa mtumishi anaitwa Prisca alikuja 28/10/2016 na saini yake ipo ofisini kwenye kitabu alipokuja kuripoti, baadae tuliambiwa ameondolewa kwa sababu ya vyeti feki,” alisema.
Naye Mwenyekiti wa Kijiji hicho, Idd Baba, alisema zahanati hiyo imegeuka mzigo kwake, kwani amefanya jitihada kufuatilia ngazi za juu lakini hajapata majibu ya kuridhisha.
“Kila siku mara leo mara kesho, naletewa daktari mara tunaambiwa ni feki, naanza tena kufuatilia nikaletewa mwingine mara nikasikia naye amehamishwa,” alisema.
Diwani wa Kata ya Mrijo, Hamisi Msakati (CCM), alikiri wananchi hao kupata shida licha ya jengo kukamilika muda mrefu na kueleza kuwa alipofuatilia wilayani kuhusu watumishi aliambiwa zahanati hiyo haijasajiliwa.
“Mwaka jana walileta doctor mwingine alikuja akaripoti nikapata na barua, lakini mazingira aliyoondokea ni ya kutatanisha. Nilipofuatilia wilayani Mganga Mkuu wa Wilaya akaniambia hii zahanati haijasajiliwa.
“Nilimwambia kuna watumishi wawili mmewaleta kule, wakati mnafanya hayo hili la usajili mlikuwa hamlijui? Kwa kweli sikupata majibu ya kuridhisha, hayatoshelezi hata kwa akili za kawaida,” alisema.
Mwandishi alilazimika kumtafuta Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, Dk. Semistatus Mashimba,  ambaye alishangazwa na taarifa hizo na kuahidi kuchukua hatua mara moja ili wananchi hao wapate huduma.
“Hili ndiyo nalisikia kutoka kwako, kwanza nikushukuru kwa kunipa taarifa hili nalifuatilia kuanzia sasa, yaani hata diwani ameshindwa kufika ofisini kwangu hata simu ameshindwa kunipigia tukalimaliza?
“Miaka minne watu hawapati huduma na jengo limekamilika kama ni usajili taratibu zake zipo wazi kinachokwamisha ni nini? Uzembe huu hauwezi kuvumiliwa,” alisema Dk. Mashimba.

Post a Comment

Previous Post Next Post