Nteghenjwa Hosseah, OR-TAMISEMI.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala
za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe.
Selemani Jafo amewataka Wakuu wote wa Mikoa na Wilaya Nchini kuhakikisha wanaanzisha
kituoa kimoja cha huduma ‘One Stop Center’ kwa ajili ya
wawekezaji.
Mhe. Jafo ameyasema hayo wakati wa
ufunguzi wa Warsha ya namna ya Uendeshaji wa Mabaraza ya Biashara kwa Mikoa na Halmashauri
zote Nchini iliyoandaliwa na Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Ofisi
ya Waziri Mkuu pamoja na Mradi wa Local Investiment Climate (LIC)
inayofanyika kwa siku mbili Jijini Dodoma.
Katika Warsha hiyo inayowajumuisha
viongozi wa Ngazi za Mkoa na Wilaya Mhe.
Jafo amesema mazingira magumu ya upatikanaji wa taarifa za uwekezaji na
urasimu uliopo katika Mikoa na Wilaya ndio unaowakwaza Wawekezaji katika
harakati zao za kutaka kuwekeza katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.
“Imekuwa ni vigumu sana kwa
Muwekezaji kupata taarifa sahihi na kwa wakati katika maeneo yetu na hii imekua
ikiwakatisha moyo na kupelekea hata kusitisha mpango mzima na nia yao ya
kuwekeza katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, inatakiwa tubadilike na tuweke
mazingira rahisi yatakayomuweza kila mdau anayetaka kuwekez kupata taarifa
anazozihitaji kwa urahisi.
Hali hii inarudisha nyuma juhudi zetu
za kuhamasisha uwekezaji sasa basi kila kiongozi wa Mkoa na Wilaya kuhakikisha
wanaanzisha kituo kimoja “One Stop Center” ambacho kitatoa
huduma zote kwa Wawekezaji kama vile upatikanaji wa maeneo ya uwekezaji, Leseni
za biashara, Hati miliki, usajili wa kampuni, namna ya ulipaji wa kodi nk”
alisema Jafo.
Aliongeza kuwa warsha hii
imewakutanisha wadau kutoka Sekta ya umma na binafsi katika kila ngazi ya
utawala ili kujadiliana namna bora ya kuboresha mazingira ya biashara na
uwekezaji Nchini na hivyo basi ni wakati wa kukubaliana kwa pamoja namna
mabaraza ya Biashara yatakavyosaidia katika kukuza Uchumi wa Viwanda ambao ndio
muelekeo wetu kama Taifa kwa hivi sasa.
Sambamba na hilo Jafo aliwakumbusha
viongozi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuwa pamoja na majukumu mengine
wanapaswa kutengeneza mazingira bora ya kufanyia biashara na uwekezaji, kuibua
fursa za uwekezaji, kuzinadi fursa zilizoibuliwa kupitia Makongamano ya
uwekezaji na kuandaa midahalo mahususi.
Pia Mhe. Jafo alisisitiza kuwa mara
baada ya kikao hiki kila kiongozi akahakikishe kuwa Vikao vya mabaraza ya
Biashara vinafanyika kwa mujibu wa Sheria na viongozi washiriki katika vikao
hivyo na maazimio ya vikao hivyo yakashughulikiwe kwa wakati na kutoa mrejesho
kwa upande wa sekta za umma na binafsi.
Aidha kila Halmashauri zikatenge
bajeti kwa ajili ya uendeshaji wa Mabaraza ya biashara na kwa upande wa Sekta binafsia ziandae
utaratibu mzuri wa kuchangia gharama za uendeshaji wa vikao hivyo.
Alimalizia kuwa Mradi wa LIC kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais
TAMISEMI pamoja na Baraza la Taifa la Biashara kuandaa utaratibu wa kueneza
uzoefu uliopatikana katika Mikoa miwli ya Dodoma na Kigoma ambapo mradi huu
umetekelezwa ili mikoa mingine iweze kujifunza na kuboresha mazingira ya
biashara na uwekezaji.
Mabaraza ya Biashara Tanzania
yameanzishwa kwa mujibu wa Waraka wa Rais Na. 1 wa mwaka 2001 na kuchapishwa
kwenye Gazeti la Serikali Na. 691 la tarehe 28 Seot,2001.
Waziri
wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo akifungua warsha ya kujadili changamoto za
Uendeshaji wa Mabaraza ya Biashara Tanzania inayofanyika kwa siku mbili Jijini
DodomaMkuu wa Mkoa wa Dodoma Mhe. Dkt. Bilinith Mahenge akizungumza na wadau wa baraza la biashara kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kufungua warsha hiyo.
1. Mkurugenzi Msaidia wa
Utawala toka OR-TAMISEMI Bw. Mrisho Mrisho akiongoza warsha ya Mabaraza ya
Biashara Tanzania.
1Mshauri wa Majadiliano
baina ya Sekta Umma na Binafsi wa LIC Bw.
Donald Liya (Kwanza kushoto)
akifuatiwa na Kiongozi Msaidizi wa Timu ya LIC
Bw. Peter Laizer, Mshauri wa Mradi wa LIC toka Taasisi ya Sekta Binafsi Bi. Rehema Mbugi pamoja na Kaimu
Mkurugenzi wa TCCIA Bw. Gotfried Muganda
wakifuatilia warsha ya kujadili changamoto ya Uendeshaji wa Mabraza ya
Biashara.